56

Kumtumainia Mungu
(Kwa Mwimbishaji: Mtindo “Njiwa Mkimya wa Mbali”. Utenzi wa Daudi baada ya kukamatwa na Wafilisti kule Gathi)
1 Ee Mungu, unionee huruma, maana watu wananishambulia. Mchana kutwa maadui wananidhulumu.
2 Mchana kutwa maadui zangu wananishambulia; ni wengi mno hao wanaonipiga vita.
3 Ee Mungu Mkuu, hofu inaponishika, mimi nakutumainia wewe.
4 Namtumainia Mungu na kusifu neno lake; namtumainia Mungu, wala siogopi. Binadamu dhaifu atanifanya nini?
5 Mchana kutwa wanapotosha kisa changu; mawazo yao yote ni ya kunidhuru.
6 Wanakutana kupanga na kunivizia; wanachunguza yote nifanyayo; wananiotea kwa shabaha ya kuniua.
7 Ee Mungu, uwalipe kwa kadiri ya uovu wao, uwaangushe hao waovu kwa hasira yako.
8 Wewe wakujua kusukwasukwa kwangu; waweka kumbukumbu ya machozi yangu yote. Je, yote si yamo kitabuni mwako?
9 Kila mara ninapokuomba msaada wako, maadui zangu wanarudishwa nyuma. Najua kweli Mungu yuko upande wangu.
10 Namtumaini Mungu na kusifu neno lake; namtumainia Mwenyezi-Mungu na kusifu neno lake.
11 Namtumainia Mungu, wala siogopi. Binadamu atanifanya nini?
12 Ee Mungu, nitatimiza ahadi zangu kwako; nitakutolea tambiko za shukrani,
13 Maana umeniokoa katika kifo, naam, umenilinda nisianguke chini; nipate kuishi mbele yako, ee Mungu, katika mwanga wa uhai.

Generic placeholder image