52

Hukumu ya Mungu
(Kwa Mwimbishaji. Utenzi wa Daudi baada ya Doegi, Mwedomu, kumwendea Shauli na kumjulisha kuwa Daudi amekwenda nyumbani kwa Abimeleki)
1 Mbona, ewe jitu, wajivunia ubaya wako dhidi ya wenye kumcha Mungu?
2 Kila wakati unawaza maangamizi; ulimi wako ni kama wembe mkali! Unafikiria tu kutenda mabaya.
3 Wewe wapenda uovu kuliko wema, wapenda uongo kuliko ukweli.
4 Ewe mdanganyifu mkuu, wapenda mambo ya kuangamiza wengine.
5 Kwa hivyo Mungu atakuangamiza milele, atakunyakua na kukuondoa nyumbani mwako; atakungoa katika nchi ya walio hai.
6 Waadilifu wataona hayo na kuogopa, kisha watakucheka na kusema:
7 “Tazameni yaliyompata mtu huyu! Yeye hakutaka Mungu awe kimbilio lake; bali alitegemea wingi wa mali yake, na kutafuta humo usalama wake!”
8 Lakini mimi ni kama mzeituni mbichi, unaostawi katika nyumba ya Mungu. Nazitegemea fadhili zake milele na milele.
9 Ee Mungu, nitakushukuru daima, kwa ajili ya mambo uliyofanya. Nitatangaza kwamba wewe ni mwema, mbele ya watu wako waaminifu.

Generic placeholder image