KUPAA BWANA MWAKA B
MASOMO

ANTIFONA YA KUINGIA: Mdo.1:11
Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Yesu atakuja jinsi hiyohiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni, aleluya!

Utukufu husemwa.

KOLEKTA

Ee Mungu mwenyezi, utufanye tufurahi kwa furaha takatifu, na kuchangamka kwa tendo la ibada ya shukrani, kwani kupaa kwake Kristo Mwanao ni kuinuliwa kwetu; na kule alikotutangulia yeye kichwa chetu, kwa utukufu, hukohuko twatumaini kuweko pia sisi mwili wake. Kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, milele na milele.

Au:
Ee Mungu mwenyezi, sisi tunasadiki kwamba leo Mwanao pekee Mkombozi wetu amepaa mbinguni. Tunakuomba utujalie nasi pia tuwe tunaishi mbinguni kiroho. Kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, milele na milele.

SOMO 1: Mdo.1:1-11
Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi. Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao. Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.47:1-2,5-6,7-8(K)5
1. Enyi watu wote, pigeni makofi,
Mpigieni Mungu kelele kwa Sauti ya shangwe.
Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya,
Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote.

(K) Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,
Bwana kwa sauti ya baragumu.
Au:
Aleluya.

2. Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,
Bwana kwa sauti ya baragumu.
Mwimbieni Mungu, naam, imbeni;
Mwimbieni mfalme wetu, naam, imbeni. (K)

3. Maana Mungu ndiye mfalme wa dunia yote,
Imbeni kwa akili.
Mungu awamiliki mataifa,
Mungu ameketi katika kiti chake kitakatifu. (K)

SOMO 2: Efe.1:17-23
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.

SHANGILIO: Mt.28:19-20
Aleluya, aleluya!
Basi, enendeni,
mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi,
na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote
Aleluya!

INJILI: Mk.16:15-20
Yesu alionekana na wale kumi na mmoja, akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya. Basi Bwana Yesu, baada ya kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.

Nasadiki husemwa.

MAOMBI
Tumwombe Bwana Yesu Kristo aliyeketi kuume kwa Mungu Baba kama mshindi, mwombezi na mtetezi wetu mkuu.

Ee Bwana Yesu Kristo,
1. Uliwatuma mitume duniani wawe mashahidi wako. Utupe sisi moyo wa kukushuhudia katika kazi na shughuli zetu za kila siku.

2. Ulisema: Aaminiye ataokoka: Utuongoze kutumia mambo ya dunia kwa imani.

3. Uliwaahidi mitume kwamba hawatapatwa na madhara katika kutimiza ujumbe wako. Utujalie ulinzi wako katika hatari tunazokumbana nazo maishani.

4. Uliwapa mitume wako nguvu ya kuponya. Utupe sisi neema ya kuwasaidia wagonjwa wetu, tuwatunze yatima na kuwasindikiza walio mahututi.

5. Uliwapa mitume wako amani yako. Uwasaidie wenye madaraka kukomesha vita, wazime njaa na kuwaondolea watu hofu.

Ee Mungu, Mwana wako alitawazwa mbinguni ashike usukani mikononi mwake. Usikilize maombi yetu kwa njia yake Yeye anayeishi pamoja na daima na milele. Amina.

SALA YA KUOMBEA DHABIHU
Ee Bwana, tunakutolea kwa unyenyekevu sadaka hii, kwa heshima ya kupaa kwake Mwanao. Tunakuomba utujalie ili, kwa njia ya mabadilishano haya matakatifu ya vipaji, tupate kuinuliwa hadi mambo ya mbinguni. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu.

ANTIFONA YA KOMUNYO: Mt.28:20
Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari, aleluya!

SALA BAADA YA KOMUNYO
Ee Mungu mwenyezi wa milele, wewe unatujalia tuliopo hapa duniani tuweze kuyashughulikia mambo ya mbinguni. Tunakuomba uuelekeze moyo wa ibada Wa sisi wakristo huko aliko Bwana Yesu, aliyechukua ubinadamu wetu. Anayeishi na kutawala milele na milele.