JUMATATU JUMA LA 3 PASAKA
MASOMO
SOMO: Mdo.2:14,22-32
Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini
baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia,
na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana
na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, tumemsikia mtu huyu
akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi;
wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema,
Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana
tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahli hapa, na kuzibadili desturi
tulizopewa na Musa. Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso
wake kuwa kama uso wa malaika.
WIMBO WA KATIKATI: ZAB.119:23-24,26-27,29-30(K)1
1. Wakuu nao waliketi wakaninena,
Lakini mtumishi wako atazitafakari amri zako.
Shuhuda zako ndizo furaha yangu,
Na washauri wangu.
(K) Heri walio kamili njia zao.
2. Nalizisimulia njia zangu ukanijibu,
Unifundisha amri zako.
Unifahamishe njia ya mausia yako,
Nami nitayatafakari maajabu yako. (K)
3. Uniondolee njia ya uongo,
Unineemesha kwa sheria yako.
Nimeichagua njia ya uaminifu,
Na kuziweka hukumu zako mbele yangu. (K)
SHANGILIO: Lk.24:25-26
Aleluya, aleluya,
Ilimpasa Kristu kupata mateso haya,
na kuingia katika utukufu wake.
Aleluya.
INJILI: Yn.6:22-29
Siku ya pili yake mkutano waliosimama ng’ambo ya bahari waliona ya kuwa hakuna mashua nyingine
huko ila moja; tena ya kuwa Yesu hakuingia katika mashua ile pamoja na wanafunzi wake, bali
wanafunzi wake walikwenda peke yao. Walakini zikaja mashua nyingine kutoka Tiberia mpaka karibu
na mahali pale walipokula mikate, wakati Bwana aliposhukuru. Basi mkutano, walipoona ya kuwa Yesu
hayuko huko wala wanafunzi wake, waliingia mashuani wenyewe, wakaenda Kapernaumu wakimtafuta Yesu.
Hata walipomwona ng’ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa? Yesu akawajibu,
akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu
mlikula ile mikate mkashiba. Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho
hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na
Baba, yaani, Mungu. Basi wakamwambia, Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? Yesu akajibu,
akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye.
MAOMBI
Ndugu, mkutano wa watu ulimfuata Yesu hata ukamkuta ng'ambo ya bahari kwa sababu kabla yake
aliwapa mikate wakashiba. Hata sisi tunahitaji msaada wa Mungu tupate kuwa mashahidi waaminifu
wa Injili yake. Basi, tuombe.
Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Uwape viongozi wetu wa Kanisa neema na uwezo wa kuwa mfano bora katika kufanya maajabu na
ishara kubwa katika watu wanaowaongoza.
2. Uzuie ushindani usio na manufaa yoyote kimwili au kiroho kati ya mataifa, ili watu waufuate
ukweli wako.
3. Sisi sote tuzitende kazi zako, Ee Mungu, kwa kumwamini mwanao uliyemtuma kwetu.
4. Uwahesabie haki marehemu wetu wapate kung'ara mbele yako kama uso wa malaika.
Ee Baba yetu mwema, utudumishe katika kuepa kufuru za mambo matakatifu, tukashike amri zako na
desturi zile tu ambazo zinakubalika mbele yako. Kwa Kristo Bwana wetu. Amina.