JUMATATU JUMA 21 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: 1The.1:2-5,8-10
Twamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu. Wala hatuachi kuikumbuka kazi yenu ya imani, na taabu yenu ya upendo, na saburi yenu ya tumaini lililo katika Bwana wetu Yesu Kristo, mbele za Mungu Baba yetu. Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, twajua uteule wenu; ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu. Maana kutoka kwenu neno la Mungu limevuma, si katika Makedonia na Akaya tu, ila na kila mahali imani yenu mliyo nayo kwa Mungu imeenea; hata hatuna haja sisi kunena lo lote. Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli; na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.149:1-6 (K)4
1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyiko la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao.

(K) Bwana awaridhia watu wake.

2. Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake,
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

3. Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote. Aleluya. (K)

SHANGILIO: Zab.130:5
Aleluya, aleluya!
Roho yangu inamngoja Bwana,
na neno lake nimelitumainia.
Aleluya!

INJILI: Mt.23:13-22
Yesu aliwaambia makutano na wafuasi wake: Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie. Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanumu mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe. Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga. Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au ile hekalu liitakasalo dhahabu? Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo juu yake, amejifunga. Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu iitakasayo sadaka? Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo juu yake. Naye aapaye kwa hekalu, huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake. Naye aapaye kwa mbingu, huapa kwa kiti cha enzi cha Mungu, na kwa yeye aketiye juu yake.

--------------

--------------
MAOMBI
Ndugu, Bwana Mungu ni mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli. Tumwombe.

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Uwape viongozi wetu wa Kanisa karama ya kuwafariji waamini wao wapatwapo na mashaka au misukosuko katika imani yao kwako. Ee Bwana.

2. Watu wa mataifa yote wakuongokee na kukutumikia Wewe Mungu uliye hai na wa kweli, wakiacha sanamu na yote yanayopingana na jina lako. Ee Bwana.

3. Wabatizwa wote tujaliwe neema ya kulihubiri na kuliishi neno lako, lipate kuvuma kote na kuwaokoa wengi. Ee Bwana.

4. Tunawaombea wote wanaoteseka kwa ajili ya jina lako, ili wahesabiwe haki na kila tunda la imani yao wapate kuingia katika ufalme wako wa mbinguni. Ee Bwana.

5. Uwarehemu marehemu wetu na kuwaingiza katika ufalme wako huko mbinguni. Ee Bwana

Ee Mungu unayetukuzwa kwa sala na matendo yetu uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.