JUMATATU JUMA 15 LA MWAKA WA 1
MASOMO
SOMO 1: Kut.1:8-14,22
Aliinuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi, tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka;
tena, kukitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika
nchi hii, Basi wakaweka wasimamizi juu yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya
kuwekea akiba, Pithomu na Ramesesi. Lakini kwa kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka na
kuzidi kuenea. Nao walichukiwa kwa sababu ya wana wa Israeli. Wamisri wakawatumikisha wana wa Israeli
kwa ukali; wakafanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali, na kila
namna ya kazi ya mashamba; kwa kazi zao zote walizowatumikisha kwa ukali. Kisha huyo Farao akawaagiza
watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke
mtahifadhi hai
WIMBO WA KATIKATI: Zab.124 (K)8
1. Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi,
Israeli na aseme sasa,
Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi
wanadamu walipotushambulia.
Papo hapo wangalitumeza hai,
Hasira yao ilipowaka juu yetu.
(K) Msaade wetu u katika jina la Bwana.
2. Papo hapo maji yangalitugharikisha,
Mto ungalipita juu ya roho zetu.
Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu
Maji yafurikayo. (K)
3. Na ahimidiwe Bwana:
Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno hayo.
Nafsi yetu imeokoka kama ndege
Katika mtego wa wawindaji,
Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. (K)
SHANGILIO: 1Sam.3:9/ Yn.6:68
Aleluya, aleluya!
Nena Bwana,
kwa kuwa mtumishi wako anasikia:
wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya!
INJILI: Mt.10:34-11:1
Yesu aliwafundisha mitume wake: Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja
kuleta amani, bali upanga. Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye,
na mkwe na mkwe mtu; na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake. Apendaye baba au mama kuliko
mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili. Wala mtu asiyechukua
msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza
nafsi yake kwa ajili yangu ataiona. Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea
yeye aliyenituma. Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye
mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki. Na mtu awaye yote atakayemnywesha
mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia,
haitampotea kamwe thawabu yake. Ikawa Yesu alipokwisha kuwaagiza wanafunzi wake kumi na wawili,
alitoka huko kwenda kufundisha na kuhubiri katika miji yao.
--------------
--------------
MAOMBI
Ndugu zangu, tuyaelekeze maombi yetu kwa Mungu aliyejifunua
katika nafsi tatu tukisema.
Kiitikio: Upokee ombi letu.
1. Uwajalie Maaskofu na wachungaji wote wa Kanisa lako ari
ya kuendeleza kazi ya unabii katika dunia hii, hasa pale
palipojaa machafuko na itikadi potofu. Ee Bwana.
2. Uendelee kuiamsha busara ndani ya viongozi wote wa dunia;
wazidi kuwa waamuzi wenye haki, na daima waitegee masikio
sheria yako. Ee Bwana.
3. Uwatie moyo wanaharakati wote wanaojibidisha katika
kutetea haki, amani na usawa kwa binadamu wote. Ee Bwana.
4. Wote wakuaminio wakupende zaidi ya chochote, kiasi
cha kuwa tayari kupoteza nafsi zao kwa ajili yako. Ee Bwana.
5. Marehemu wetu watakaswe dhambi zao na kuzawadiwa
uzima wa milele huko mbinguni. Ee Bwana.
Ee Mungu unayetaka tukupende zaidi ya chochote, uyapokee
maombi yetu kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.