JUMATANO JUMA 30 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Rum.8:26-30
Roho hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu. Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.13:3-6 (K)5
1. Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti. Adui yangu asije akasema, Nimemshinda; Watesi wangu wasifurahi ninapoondoshwa.

(K) Nimezitumainia fadhili zano, Ee Bwana.

2. Nami nimezitumainia fadhili zako; Moyo wangu na uufurahie wokovu wako. Naam, nimwimbie Bwana, Kwa kuwa amenitendea kwa ukarimu. (K)

SHANGILIO: 1The.2:13
Aleluya, aleluya!
Lipokeeni neno la Mungu mliusikia, mkaupokea,
si kama vile ujumbe wa binadamu,
bali kama ujumbe wa Mungu,
na kweli ndivyo ulivyo.
Aleluya!

INJILI: Lk.13:22-30
Yesu alikuwa akipita katika miji na vijiji, akifundisha, katika safari yake kwenda Yerusalemu. Mtu mmoja akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akamwambia, Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia wasiweze, wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako; ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. Naye atasema, Nawaambia, siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu. Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje. Nao watakuja watu toka mashariki na magharibi, na toka kaskazini na kusini, nao wataketi chakulani katika ufalme wa Mungu. Na tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.

--------------

--------------
MAOMBI
Ee Mungu, katika mambo yote Wewe hufanya kazi pamoja na wale wakupendao katika kuwapatia mema. Kwa hiyo tunathubutu kukuomba tukisema:-

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Upende kumjalia Askofu wetu F. mafanikio katika kazi zake za kichungaji, na umuimarishe katika upendo. Ee Bwana.

2. Uwajalie watu wako utii kwa wenye mamlaka; kwani kila neno jema alitendalo mtu yeyote ndilo atakalopewa nawe. Ee Bwana.

3. Watu wote wajaliwe kuufahamu ukweli huu, kwamba kukujua Wewe ni kutenda mema na kuachana na udhalimu. Ee Bwana.

4. Roho wako atusaidie katika udhaifu wetu, kwa maana mara nyingi hatujui kuomba itupasavyo. Ee Bwana.

5. Roho wako awatakase marehemu wetu na kuwapa uzima mpya huko mbinguni. Ee Bwana.

Ee Mungu, tunakuletea maombi haya kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.