JUMATANO JUMA 27 LA MWAKA WA 1
MASOMO
SOMO 1: Yon.4:1-11
Yona alikasirika sana. Akamwomba Bwana, akasema, Nakuomba, Ee Bwana; sivyo hivyo nilivyosema, hapo
nilipokuwa katika nchi yangu? Hii ndiyo sababu nalifanya haraka kukimbilia Tarshishi; kwa maana
nalijua ya kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema,
nawe waghairi mabaya. Basi, sasa, Ee Bwana, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana ni afadhali
nife mimi kuliko kuishi. Naye Bwana akasema, Je! Unatenda vema kukasirika? Ndipo Yona akatoka
mjini, akaketi upande wa mashariki wa mji, akajifanyia kibanda huko, akakaa chini yake uvulini,
hata aone mji ule utakuwaje. Na Bwana Mungu aliweka tayari mtango, akaufanya ukue juu ya Yona,
ili uwe kivuli juu ya kichwa chake, na kumponya katika hali yake mbaya. Basi Yona akafurahi sana
kwa sababu ya ule mtango. Lakini siku ya pili kulipopambazuka, Mungu akaweka tayari buu, nalo
likautafuna ule mtango, ukakatika. Basi ikawa, jua lilipopanda juu, Mungu akaweka tayari upepo wa
mashariki, wenye hari nyingi; jua likampiga Yona kichwani, hata akazimia, naye akajitakia kufa,
akasema, Ni afadhali nife mimi kuliko kuishi. Mungu akamwambia Yona, Je! Unatenda vema kukasirika
kwa ajili ya mtango? Naye akasema, Ndiyo, natenda vema kukasirika hata kufa. Bwana akamwambia,
Wewe umeuhurumia mtango, ambao hukuufanyia kazi, wala kuuotesha; uliomea katika usiku mmoja, na
kuangamia katika usiku mmoja; na mimi, je! Haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao
ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia
na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?
WIMBO WA KATIKATI: Zab.86:3-6,9-10 (K)5
1. Wewe, Bwana, unifadhili,
Maana nakulilia Wewe mchana kutwa.
Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,
Maana nafsi yangu nakuinulia Wewe, Bwana.
(K) Wewe Bwana, u Mungu wa rehema na neema.
2. Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema,
Umekuwa tayari kusamehe,
Na mwingi wa fadhili, Kwa watu wote wakuitao.
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu;
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)
3. Mataifa yote uliowafanya watakuja;
Watakusujudia Wewe, Bwana,
Watalitukuza jina lako;
Kwa kuwa ndiwe uliye mkuu,
Wewe ndiwe mfanya miujiza,
Ndiwe Mungu peke yako. (K)
SHANGILIO: Ebr.4:12
Aleluya, aleluya!
Neno la Mungu li hai tena li na nguvu,
li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.
Aleluya!
INJILI: Lk.11:1-4
Yesu alipokuwa mahali fulani akiomba, alipokwisha, mmoja katika wanafunzi wake alimwambia,
Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile Yohane alivyowafundisha wanafunzi wake. Akawaambia,
Msalipo, semeni: Baba, Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, Utupe siku kwa siku riziki yetu.
Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni.
--------------
--------------
MAOMBI
Wapendwa, Mungu ni mwenye neema, amejaa huruma, si
mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema; naye hughairi
mabaya. Tumwombe:-
Kiitikio: Pokea ombi letu.
1. Wachungaji na wahubiri wote wa neno lako wafurahie
kazi yao waonapo wakosefu wanatubu na kukuongokea Wewe. Ee Bwana.
2. Ufalme wako uje katika ulimwengu huu uliojaa
maovu, ili watu wako waondokane na ubinafsi na mambo yote
ya anasa za dunia. Ee Bwana.
3. Umjalie kila mmoja wetu moyo wa sala katika
mazingira yoyote: katika majaribu, katika mashaka,
katika taabu na hata katika raha. Ee Bwana.
4. Utuepushe na woga au unafiki katika utume wetu,
ili ukweli wa neno lako upate kuhubiriwa bila ubaguzi kwa
watu wote na katika mazingira yoyote. Ee Bwana.
5. Kwa huruma yako, marehemu wetu waione nuru
ya uso wako mtukufu huko mbinguni. Ee Bwana.
Ee Mungu unayefurahi kuona wakosefu wanatubu na kukurudia Wewe,
uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.