JUMATANO JUMA 24 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: 1Tim.3:14-16
Nakuandikia hayo, nikitaraji kuja kwako hivi karibu. Lakini nikikawia, upate kujua jinsi iwapasavyo watu kuenenda katika nyumba Mungu, iliyo kanisa la Mungu aliye hai, nguzo na msingi wa kweli. Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu: Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.111:1-6 (K)2
1. Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote, Barazani pa wanyofu wa moyo na katika mkutano. Matendo ya Bwana ni makuu. Yafikiriwa sana na wapendezwao nayo.

(K) Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao.

2. Kazi yake ni heshima na adhama, Na haki yake yakaa milele. Amefanya ukumbusho wa matendo yake ya ajabu; Bwana ni mwenye fadhili na rehema. (K)

3. Amewapa wamchao chakula; Atalikumbuka agano lake milele. Amewajulisha watu wake uwezo wa matendo yake, Kwa kuwapa urithi wa mataifa. (K)

SHANGILIO: Lk.6:63,68
Aleluya, aleluya!
Maneno yako, Bwana, ni roho na uzima.
Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya!

INJILI: Lk.7:31-35
Yesu aliwaambia makutano: Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia. Kwa kuwa Yohane Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, ana pepo. Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. Na hekima imejulikana huwa ina haki kwa watoto wake wote.

--------------

--------------
MAOMBI
Ndugu, kanisa ni nyumba ya Mungu na mahali rasmi pa kukutana na kuongea naye. Kwa vile yupo tayari kutusikiliza, tumwombe.

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Uwajalie wachungaji wetu udumifu katika kuwaelekeza kwa upole watu wote, kuitikia mwito wa kulitunza na kulitumia vema kanisa lako. Ee Bwana.

2. Ubariki juhudi za viongozi wa serikali, asasi na taasisi zake, katika kutimiza amri yako ya upendo kwa watu wote. Ee Bwana.

3. Wote waliojitenga nawe na wenye dhambi wajaliwe moyo wa kumkaribia Mwanao, Yesu Kristo, aliyekuja kwa ajili yao. Ee Bwana.

4. Sisi sote tujaliwe kuijua siri kuu ya utaua, tupate kukudhihirisha na kukuhubiri kwa mataifa, ili nao wapate kukuamini na kuokoka. Ee Bwana.

5. Marehemu wetu wapokelewe huko mbinguni na kupewa uzima wa milele. Ee Bwana.

Ee Mungu uliyetaka hekima ijulikane kuwa ina haki kwa watoto wake wote, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.