JUMATANO JUMA 19 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Kum.34:1-12
Musa alipanda kutoka uwanda wa Moabu mpaka mlima Nebo, hata kilele cha Pisga kukabili Yeriko. Bwana akamwonyesha nchi yote ya Galiadi hata Dani; na Naftali yote, na nchi ya Efraimu na Manase, na nchi yote ya Yuda, mpaka bahari ya magharibi; na Negebu, na uwanja wa bonde la Yeriko, mji wa mitende, hata mpaka Soari. Bwana akamwambia, Hii ndiyo nchi niliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, nikisema, Nitawapa wazao wako. Basi nimekuonyesha kwa macho yako, lakini hutavuka huko. Basi Musa, mtumishi wa Bwana, akafa huko, katika nchi ya Moabu, kwa neno la Bwana. Akamzika bondeni, katika nchi ya Moabu, kukabili Beth-peori; lakini hapana mtu ajuaye kaburi lake hata leo. Musa alikuwa mtu wa miaka mia na ishirini alipokufa; jicho lake halikupofuka, wala nguvu za mwili wake hazipunguka. Wana wa Israeli wakamwomboleza Musa katika uwanda wa Moabu siku thelathini; basi siku za maombolezo ya matanga ya Musa zikaisha. Na Yoshua. mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyowamuru Musa. Musa, hajainuka tena katika Israeli nabii kama Musa, ambaye Bwana alimjua uso kwa uso; katika ishara zote na maajabu yote, ambayo Bwana alimtuma kuyatenda katika nchi ya Misri, kwa Farao, na kwa watumishi wake wote, na kwa nchi yake yote; na katika ule mkono wa nguvu wote, katika ule utisho mkuu wote, alioutenda Musa machoni pa Israeli wote.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.66:1-3,5,8,16-17 (K)20:9
1. Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote, imbeni utukufu wa jina lake, tukuzeni sifa zake. Mwambieni Mungu: Matendo yako yatisha kama nini.

(K) Ahimidiwe Mungu, aliyeweka nafsi yetu katika uhai.

2. Njani yatazameni matendo ya Mungu, Hutisha kwa mambo awetendayo wanadamu. Enyi mataifa, mtukuzeni Munug wetu, itangazeni sauti ya sifa zake. (K)

3. Njoni sikieni, ninyi nyotc mnaomcha Mungu, nami nitayatangaza alivyonitendea roho yangu. Nalimwita kwa kinywa changu, na sifa kuu zilikuwa chini ya ulimi wangu. (K)

SHANGILIO: 2Kor.5:19
Aleluya, aleluya!
Mungu alikuwa ndani ya Kristu,
akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake
ametia ndani yetu neno la upatanisho.
Aleluya!

INJILI: Mt.18:15-20
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru. Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.

--------------

--------------
MAOMBI
Ee Mungu, Mwanao Yesu Kristo ametuhakikishia kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina lake, naye yupo papo hapo katikati yao. Basi, tunakuomba:-

Kiitikio: Pokea ombi letu.
1. Uwajalie afya na nguvu Baba Mtakatifu na Maaskofu wetu wote; uwakirimie roho ya hekima, wapate kulichunga vema kundi lako. Ee Bwana.

2. Uwajalie daima watu wako viongozi waadilifu na wenye bidii, ili wasibaki kama kondoo wasio na mchungaji. Ee Bwana.

3. Umjalie kila mmoja wetu busara katika kutatua matatizo yanayojitokeza katika jamii zetu; ili haki itendeke na upendo wa kweli utawale jumuiya zetu. Ee Bwana.

4. Usikilize dua za watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika duniani; na uwaokoe wazee, vijana na watoto wanaokutumainia. Ee Bwana.

5. Marehemu wetu wasamehewe dhambi zao na kuurithi uzima wa milele. Ee Bwana.

Ee Mungu, tunaamini kuwa wanaopatana duniani katika jambo lolote wanaloliomba kwako watafanyiwa. Uyapokee maombi yetu kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.