JUMATANO JUMA 15 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Kut.3:1-6,9-12
Musa alikuwa akilichunga kundi la Yethro mkwewe, kuhani wa Midiani; akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpaka mlima wa Mungu, hata Horebu. Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea. Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei. Bwana alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa. Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapa unaposimama ni nchi takatifu. Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu. Bwana akasema: Tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri? Akasema, Bila shaka mimi nitakuwa pamoja nawe; na dalili ya kuwa nimekutuma ndiyo hii; utakapokuwa umekwisha kuwatoa hao watu katika Misri, mtamwabudu Mungu katika mlima huu.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.103:1-4,6-7 (K)8
1. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Naam vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote.

(K) Bwana amejaa huruma na neema.

2. Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote. Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

3. Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki, Na hukumu kwa wote wanaoonewa. Akimjulisha Musa njia zake, Wana wa Israeli matendo yake. (K)

SHANGILIO: Zab.19:8
Aleluya, aleluya!
Amri ya Bwana ni safi,
huyatia macho nuru.
Aleluya!

INJILI: Mt.11:25-27
Wakati ule Yesu alijibu akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na yenyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.

--------------

--------------
MAOMBI
Ee Mungu uliyemwambia Musa: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, "twakuomba:-

Kiitikio: Upokee ombi letu.
1. Umjalie Askofu wetu F. na Mapadre wote kudumu katika kutimiza kiaminifu viapo vyao vya utii; na hivi kuwa tayari kuwahudumia kondoo wako kwa upendo usio na dosari. Ee Bwana.

2. Watawala wa dunia wajaliwe hekima na akili ya kukujua na kukuogopa Wewe Mungu wa kweli, na Mwanao wa pekee, Yesu Kristo uliyemtuma kwetu. Ee Bwana.

3. Utujalie unyenyekevu kama ule wa watoto wachanga, tupate kulipokea neno lako kwa moyo unyofu na kuliishi kwa hekima na akili. Ee Bwana.

4. Uwahurumie wenye makosa mazito; ghadhabu yako isianguke juu yao; bali uwaamshie moyo wa toba wapate kuirudia njia iliyo sawa. Ee Bwana.

5. Marehemu wetu wapokelewe nyumbani Mwako, wapate kukusifu na kukushukuru milele. Ee Bwana.

Ee Baba, Bwana wa mbingu na nchi, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.