JUMAPILI JUMA LA 6 PASAKA
MASIFU YA ASUBUHI
K. Ee Bwana, uifungue midomo yetu.
W. Nasi tutalisifu jina lako.
ANTIFONA YA MWALIKO:
Bwana amefufuka kweli, aleluya.
(K. Ant. ya Mwaliko - W. warudie Ant.)
Zab.95: Utenzi wa kumsifu Mungu
Njoni tumwimbie Mungu;
tumshangilie mwamba wa wokovu wetu!
Tuiongie kwake na nyimbo za shukrani;
tumshangilie kwa nyimbo za sifa. (W.Ant.)
Maana Mungu, ni Mungu Mkuu.
Mfalme mkuu juu ya miungu yote.
Dunia yote imo mikononi mwake,
mabonde, na vilele vya milima.
Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya;
nchi kavu kadhalika, yeye aliiumba. (W.Ant.)
Njoni tusujudu na kumwabudu;
tumpigie magoti Mungu, Mwumba wetu!
Maana yeye ni Mungu wetu!
Nasi ni watu anaowalinda,
ni kondoo wake anaowachunga. (W.Ant.)
Laiti leo mngelisikiliza anachosema:
"Msiwe na mioyo migumu kama wazee wenu kule Meriba,
kama walivyokuwa siku ile, kule Masa jangwani!
Huko wazee wenu walinijaribu na kunipima,
ingawa waliyaona mambo niliyowatendea. (W.Ant.)
Kwa miaka arobaini nilichukizwa nao,
nikasema: 'Kweli hawa ni watu waliopotoka!
Hawajali kabisa mwongozo wangu!'
Basi, nilikasirika, nikaapa:
'Hawataingia kwangu wapumzike!' (W.Ant.)
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
kama mwanzo, na sasa, na siku zote na milele.
Amina. (W.Ant.)
UTENZI chagua 1-7(25-31)
1 (25)
Kristo Bwana amefufuka!
Kila mnyororo Bwana kakata,
Sikilizeni, hao malaika
Makelele kwa shangwe wanapiga,
Milele mbinguni juu waimba,
Aleluya!
Aliyekufa kwa ajili yetu,
Na mateso mengi kuvumilia -
Kuvumilia kwa ajili yetu,
Ni Kondoo wetu wa Paska leo!
Nasi pia kwa shangwe tunaimba.
Aleluya!
Yeye aliyepata maumivu
Na hasara yote msalabani,
Sasa yupo katika utukufu,
Akitwombea, huko mbinguni,
Na anasikia kilio chetu.
Aleluya!
Sasa atuagiza tutangaze
Pote pote ulimwenguni jinsi
Ya kuokoka waliopotea,
Na ya kusamehewa wenye toba,
Na tuwezavyo ingia mbinguni.
Aleluya!
Mikaeli Weisse yapata 1480-1534
2 (26)
Aleluya! Aleluya!
Angani inatanda Pasaka!
Yesu ni mzima, hafi tena!
Giza limetokomezwa lote,
Na Bwana wa nuru Mfufuka!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Mama Maria mwone Mwanao,
Anavyofurahi kwa ushindi!
Mateso mlishiriki nyote,
Milele mtatawala nyote!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Watafuta waliopotea!
Naye Petro anakulilia!
Mwimarishe awe mwamba,
Kundi lako alichunge!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Mzima haishi kaburini,
Kristo yupo ghorofani!
Utukufu wake kauficha,
Mwili wake hai aonesha!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Japo uso wake hatuoni,
Yupo na sisi kama mwanzoni!
Ni padre wetu mtukufu,
Twashangilia mtu mzima!
Aleluya! Aleluya!
Yakobo Quinn SJ
3 (27)
Aleluya, mwimbieni Yesu,
Enzi na ufalme ni vyake.
Aleluya, fanaka ni yake,
Ushindi ni wake peke yake.
Sikizeni, nyimbo za Sion
Zinanguruma kama tufani,
Zinasikika kama gharika:
Kwa damu yake ilo azizi,
Yesu ametukomboa sisi,
Watu kutoka kila taifa.
Aleluya, katika huzuni
Kama yatima hatujaachwa;
Aleluya, yu karibu nasi,
Imani yasadiki kabisa,
Haiulizi kwa jinsi gani
Ingawa Bwana alitoweka,
Akafunikwa nayo mawingu
Siku ile ya arobaini,
Tutasahau ahadi yake:
'Nipo nanyi daima milele'?
S. S. Wesley 1810-1876
4 (28)
Kwenye Karamu ya Mwana-Kondoo
Mfalme mshindi twamwimbia,
Alotuosha kwa wingi wa maji
Kutoka penye tobo ubavuni.
Yeye analo pendo la kimungu
Waalikwa wanyweshwa damu yake,
Na awapa waule mwili wake
Pendo ndilo kafara na kuhani.
Panapomwagwa damu ya Pasaka
Mwuaji upanga aufutika;
Jeshi la Israeli lapita
Askari adui wafa maji.
Kristo kondoo aliyechinjwa,
Kafara na mkate wa Pasaka;
Tuile manna itokayo juu
Kwa unyofu na upendo halisi.
Kafara shujaa kutoka juu,
Nguvu za kuzimu ni chini yako;
Vitani mauti umeyashinda,
Uzima na mwanga kutuletea.
Bendera sasa waipeperusha,
Shetani na kaburi watiisha;
Malaika waungana kusifu
Kupinduliwa kwa bwana shetani.
Ushindi na furaha ya Pasaka
Dhambi tu ndo yaweza viharibu;
Tukinge na kifo cha dhambi Bwana,
Tulozaliwa upya ndani yako.
Tenzi za fahari, nyimbo za sifa
Tunakuimbia mpenzi Baba;
Na sifa zote milele mpate,
Bwana Mfufuka na wewe Roho.
Karne ya 7
5 (29)
Utangazeni ushindi wake,
Ewe mbingu na wewe dunia,
Maana Kristo amefufuka
Kama mwenyewe alivyosema:
Ndie yule alosulibiwa,
Ni Mungu kweli aliye hai,
Aliyekaa kwa siku tatu
Kati ya wafu huko kuzimu.
Kristo alikufa kwa aibu
Kwa ajili yetu sisi watu,
Lakini sasa aishi tena
Akiwa na nguvu na uweza;
Moto wake na haujazimwa,
Mwali wake unaoangaza
Ulimwengu wote waujaza
Kwa furaha tele na mwangaza.
Sifa na heshima kwake Baba
Ambaye hakika Hakuumbwa,
Na kwa Mwanae aliye hai
Ambaye hakika hakushindwa,
Bali anatawala kwa enzi
Pamoja na Roho wake Mungu,
Utatu ulio Mtukufu,
Katika yeye Mungu Mmoja.
Stanbrook Abbey Hymnal
6 (30)
Njoni, enyi waamini, njoni,
Mkashangilie kwa furaha;
Mungu kawapa Israeli
Furaha baada ya huzuni;
Wana na binti zake Yakobo
Si watumwa tena wa Farao;
Kawavusha miguu mikavu
Katikati ya Bahari ya Shamu.
Leo ndio roho zachipua;
Kristo jela kabomoa,
Japo siku tatu kawa mfu
Leo kachomoza kama jua;
Kipupwe chote cha dhambi zetu,
Cha muda mrefu na cha kiza,
Metokomezwa kwa yako nuru
Wewe tukusifuye daima.
Milango imara ya mauti,
Wala kaburi pana la giza,
Wala walinzi, wala muhuri,
Havikushiki uwe maiti
Maana leo ulisimama.
Kati yao Kumi na Wawili,
Amani yako ukawapatia
Ipitayo ufahamu wetu.
Mt. Yohane wa Damasko yapata 750
7 (31)
Hakika vita sasa vimekwisha,
Majeshi ya motoni yakimbia;
Tupige ukelele wa ushindi
Kwa furaha na shangwe, aleluya.
Kristo aliyeuvumilia
Ule mti utiao aibu,
Twamkaribisha tukimsifu
Aloshinda mauti, aleluya.
Asubuhi ya tatu kafufuka,
Amevishwa nuru ya utukufu.
Ambayo wenye imani thabiti
Mbinguni watavishwa, aleluya.
Ile milango duni ya kuzimu
Ufunguo wao yaachilia,
Mlango wa Paradisi u wazi;
Tusichoke kuimba, aleluya.
Bwana, kwa mapigo tulokupiga,
Tujalie tuwe mbali na kifo,
Ili tuendelee kukariri
Salamu yetu hii, aleluya.
Simphonia Sirenum 1695
ANT.I: Hii ndiyo siku iliyofanywa na Bwana, aleluya.
Zab.118 Sala ya shukrani
Huyu ndiye lile Jiwe mlilolikataa ninyi waashi, ambalo sasa limekuwa jiwe kuu la msingi
(Mate.4:11)
Mshukuruni Mungu, kwa kuwa ni mwema,*
kwa maana upendo wake mkuu ni wa milele.
Watu wa Israeli waseme:*
"Upendo wake mkuu ni wa milele.“
Wazao wa Aroni waseme:*
“Upendo wake mkuu ni wa milele."
Wote wamchao Mungu waseme:*
"Upendo wake mkuu ni wa milele."
Katika taabu yangu nilimlilia Mungu,*
naye akanisikiliza na kuniokoa.
Mungu yuko nami, siogopi kitu;*
mwanadamu atanifanya nini?
Mungu yuko nami, ananisaidia;*
nami nitashuhudia kushindwa kwa adui zangu.
Ni afadhali kumtumainia Mungu,*
kuliko kumtegemea mwanadamu.
Ni afadhali kumtumainia Mungu,*
kuliko kuwategemea viongozi wa dunia.
Watu wote wasiomjua Mungu walinizingira,*
lakini kwa nguvu ya Mungu nikawapondaponda.
Walinizunguka kila upande,*
lakini kwa nguvu ya Mungu nikawapondaponda.
Walinivamia kwa wingi kama nyuki,/
lakini wakateketea kama kichaka motoni;*
kwa nguvu ya Mungu nikawapondaponda.
Nilishambuliwa mno karibu nishindwe*
Jakini Mungu alinisaidia.
Mungu hunijalia nguvu na uhodari;*
yeye mwenyewe ameniokoa.
Sikilizeni sauti za furaha na ushindi/
katika mahema ya watu waadilifu;*
"Mkono wa Mungu umetenda mambo ya ajabu!
Mkono wa Mungu umeleta ushindi!*
Mkono wa Mungu umetenda mambo ya ajabu!"
Sitakufa, bali nitaishi,*
na kutangaza matendo ya Mungu.
Mungu ameniadhibu sana,*
lakini hakuniacha nife.
Nifungulie milango ya Hekalu;*
nitaingia na kumshukuru Mungu!
Huu ndio mlango wa Mungu,*
ambao waadilifu waweza kuupitia.
Nakushukuru, Ee Mungu, kwa kunisikiliza;*
kwa sababu wewe umeniokoa.
Jiwe walilolikataa waashi,*
limekuwa jiwe kuu la msingi.
Jambo hili limefanywa na Mungu;*
nalo ni jambo la ajabu mno kwetu.
Hi ndiyo siku aliyoifanya Mungu;*
basi, tushangilie na kufurahi.
Utuokoe, Ee Mungu, utuokoe!*
Ee Mungu, tunakusihi, utupe fanaka!
Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Mungu!*
Twakubariki kutoka nyumbani mwa Mungu.
Mungu ni Mungu, naye ni mwema kwetu./
Shikeni matawi mikononi, anzeni sherehe,*
mkiandamana mpaka madhabahuni.
Ndiwe Mungu wangu, ninakushukuru*
ninakutukuza, Ee Mungu wangu.
Mshukuruni Mungu kwa kuwa ni mwema,*
kwa maana upendo wake mkuu ni wa milele.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Ant. I: Hii ndiyo siku iliyofanywa na Bwana, aleluya.
ANT. II: Ee Bwana, Mungu wetu, umetukuzwa katika anga la mbingu;
wastahili kusifiwa milele, aleluya.
WIMBO: Dan.3:52-56 Kila kiumbe kimsifu Bwana
Mwumba astahili sifa milele (Rom.1:25)
Umehimidiwa, Ee Bwana, MUNGU wa baba zetu;*
Wastahili kusifiwa na kuadhimishwa milele.
Limehimidiwa jina lako takatifu, tukufu;*
Lastahili kusifiwa na kuadhimishwa milele.
Umehimidiwa katika hekalu la fahari yako takatifu;*
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.
Umehimidiwa juu ya kiti cha ufalme wako,*
Wastahili kusifiwa na kuadhimishwa milele.
Umehimidiwa utazamaye vilindi, uketiye juu ya makerubi;*
Wastahili kusifiwa na kuadhimishwa milele.
Umehimidiwa katika anga la mbinguni*
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.
Tumtukuze Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu;*
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.
Umehimidiwa katika anga la mbinguni,*
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.
ANT. II: Ee Bwana, Mungu wetu, umetukuzwa katika anga la mbingu;
wastahili kusifiwa milele, aleluya.
ANT. III: Mwabuduni Mungu akaaye katika kiti chake cha enzi, mkisema,
'Amina, aleluya.'
Zab.150 Zaburi ya kumsifu Mungu
Msifuni Mungu rohoni mwenu, msifuni kwa mioyo yenu, yaani: mtukuzeni Mungu kwa
roho na kwa mwili (Hesychius)
Msifuni Mungu Hekaluni mwake;*
msifuni kwa ajili ya enzi yake mbinguni.
Msifuni kwa ajili ya matendo yake makuu;*
msifuni kwa ajili ya utukufu wake mkuu.
Msifuni kwa mlio wa tarumbeta;*
msifuni kwa zeze na kinubi!
Msifuni kwa ngoma na michezo;*
msifuni kwa filimbi na bango!
Msifuni kwa kupiga matoazi;/
msifuni kwa kuvumisha matoazi.*
Kila kiumbe chenye uhai na kimsifu Mungu.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
ANT. III: Mwabuduni Mungu akaaye katika kiti chake cha enzi, mkisema,
'Amina, aleluya.'
SOMO: Mate.10:40-43
Mungu alimfufua siku ya tatu, akamfanya aonekane si kwa watu wote, ila kwa wale Mungu aliokwisha
wachagua wawe mashahidi wake, yaani sisi tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuka kwake
katika wafu. Alituamuru kuihubiri Habari Njema kwa watu wote, na kushuhudia kwamba yeye ndiye
aliyeteuliwa na Mungu awe Mwamuzi wa Wazima na wafu. Manabii wote waliongea juu yake Kwamba kila
mtu atakayemwamini atasamehewa dhambi zake zote kwa jina lake.
KIITIKIZANO
K. Utuhurumie, Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai, aleluya, aleluya. (W. Warudie)
K. Umefufuka kutoka wafu.
W. Aleluya, aleluya.
K. Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu.
W. Utuhurumie...
Ant. Wimbo wa Zakaria
Kama Baba alivyonipenda mimi, ndivyo nami nilivyowapenda ninyi. Kaeni katika pendo langu, aleluya.
WIMBO WA ZAKARIA
Lk.1:68-79 Masiha na mtangulizi wake
Asifiwe Bwana Mungu wa Israeli,/
kwani amekuja kuwasaidia*
na kuwakomboa watu wake.
Ametupatia Mwokozi shujaa,*
mzao wa Daudi, mtumishi wake.
Aliahidi hapo kale*
kwa njia ya manabii wake watakatifu,
kwamba atatuokoa kutoka maadui wetu*
na kutoka mikono ya wote wanaotuchukia.
Alisema kwamba atawaonea huruma wazee wetu,*
na kukumbuka agano lake takatifu.
Kwa kiapo alichomwapia mzee wetu Abrahamu/
aliahidi kutukomboa kutoka maadui wetu*
na kutujalia tumtumikie bila hofu,
ili tuwe watakatifu na waadilifu mbele yake*
siku zote za maisha yetu.
Nawe, mwanangu, utaitwa:*
nabii wa Mungu Aliye Juu,
utamtangulia Bwana*
kumtayarishia njia yake;
kuwatangazia watu kwamba wataokolewa*
kwa kuondolewa dhambi zao.
Mungu wetu ni mpole na mwenye huruma,/
atasababisha pambazuko angavu la ukombozi*
litujie kutoka juu,
na kuwaangazia wote wanaokaa/
katika giza kuu la kifo,*
aongoze hatua zetu katika njia ya amani.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Ant. Kama Baba alivyonipenda mimi, ndivyo nami nilivyowapenda ninyi.
Kaeni katika pendo langu, aleluya.
MAOMBI
Tumwombe Baba, Mungu Mwenyezi, aliyemfufua Kristo, mfalme wetu na Mwokozi wetu.
W. Ututukuze Bwana, kwa utukufu wa Kristo.
Baba, ulimwondoa Mwanao mpenzi kutoka giza la mauti na kumwingiza katika mwanga wa utukufu;
- utuingize katika eneo la nuru yako ya ajabu. (W.)
Ulituokoa kwa njia ya imani katika Yesu Kristo;
- utusaidie tuweze kuishi leo katika neema ya ubatizo wetu. (W.)
Umetuambia tuyatafute mambo ya mbinguni;
- utuwezeshe kuushinda mvuto wa dhambi. (W.)
Utuoneshe utajiri wa uzima wetu uliojificha katika Kristo,
- ili watu waweze kuziona ishara za mbingu mpya na dunia mpya. (W.)
Sala ya Baba yetu:
K. Na sasa tusali kwa maneno yale aliyotufundisha Mwokozi wetu:
Baba Yetu...
Baba Yetu, uliye mbinguni,
jina lako litukuzwe.
Ufalme wako ufike.
Utakalo lifanyike, duniani kama mbinguni.
Utupe leo mkate wetu wa kila siku;
utusamehe makosa yetu,
kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea,
usitutie katika kishawishi,
lakini utuopoe maovuni. Amina.
SALA:
Mungu Mwenyezi, utujalie neema ya kuadhimisha kiaminifu siku hizi za furaha zilizowekwa kwa
ajili ya heshima ya Bwana Mfufuka. Utufundishe kuzingatia kimatendo fumbo hili tunalolikumbuka
katika ibada. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, Mwanao, anayeishi na kutawala
nawe na Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele.
W. Amina.
K. Bwana atubariki, atukinge na maovu yote, na atufikishe kwenye uzima wa milele.
(W.) Amina.