DOMINIKA YA 21 YA MWAKA C
MASOMO

ANTIFONA YA KUINGIA: Zab.86:1-3
Ee Bwana, utege sikio lako unijibu. Wewe uliye Mungu wangu, umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. Wewe, Bwana, unifadhili, maana nakulilia wewe mchana kutwa.

UTUKUFU husemwa.

KOLEKTA:
Ee Mungu, wewe waiunganisha mioyo ya waamini katika nia moja. Uwawezeshe watu wako wapende unayoamuru, na kutamani unayoahidi, ili katika ulimwengu huu geugeu, mioyo yetu iwe imejikita kule kunako furaha za kweli. Kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, milele na milele.

SOMO 1: Isa.66:18-21
Bwana asema hivi: Wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu. Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa. Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka kwa Bwana, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema Bwana; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa Bwana katika chombo safi. Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi, asema Bwana.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.117, (K)Mk.16:15
1. Aleluya!
Enyi mataifa yote, msifuni Bwana,
Enyi watu wote, mhimidini

(K) Enendeni ulimwenguni mwote,
Mkaihubiri Injili.

2. Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu,
Na uaminifu wa Bwana ni wa milele. (K)

SOMO 2: Ebr.12:5-7,11-13
Ndugu zangu, mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, Wala usizimie moyo ukikemewa naye; Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi. Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani. Kwa hiyo inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe.

SHANGILIO: Yn.17:17
Aleluya, aleluya!
Maneno yako ndiyo kweli, Ee Bwana,
Ututakase sisi kwa ile kweli.
Aleluya!

INJILI: Yn.1:1-18
Yesu alikuwa akipita katika miji na vijiji, akifundisha katika safari yake kwenda Yerusalemu. Mtu mmoja akamwuliza, Je, Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akawaambia, Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze. Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako; ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. Naye atasema, Nawaambia, siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu. Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje. Nao watakuja watu toka mashariki na magharibi, na toka kaskazini na kusini, nao wataketi chakulani katika ufalme wa Mungu. Na tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.

Nasadiki husemwa.

MAOMBI
Yawezekana kwamba sisi tunabisha mlango wa mbingu na kuomba utufungulie, lakini Bwana anaweza kutuambia: siwajui ninyi. Ili kuepuka jibu la kutisha, afadhali tushike mafundisho ya Bwana.

Bwana Mungu,
1. Ututie bidii ya kupambana na magumu yaliyopo katika kufuata njia ya kuingia kwenye mlango wa mbinguni.

2. Tukumbuke kwamba maneno matupu hayatatufungulia mlango wa mbingu: Utuhimize kutekeleza imani yetu kwa matendo.

3. Uwasaidie Wakubwa wa Kanisa kuwa viongozi wa njia ya kwenda mbinguni na Uamshe wasaidizi kati ya waumini katika kazi ya uongozi na ukatekesi.

4. Uwapokee marehemu wote waliojitahidi kuhubiri Neno lako kwa maneno na matendo yao.

Ee Baba wa huruma, ulitufungulia milango ya mbinguni. Uyasikilize maombi yetu ili tupitie mlango aliotufungulia Yesu Kristo, Bwana wetu. Amina.

SALA YA KUOMBEA DHABIHU:
Ee Bwana, wewe umejipatia taifa la wanao kwa dhabihu moja idumuyo hata milele. Uwe radhi kutujalia zawadi ya umoja na amani katika Kanisa lako. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu.

ANTIFONA YA KOMUNYO: Zab.104:13-15
Ee Bwana, nchi imeshiba mazao ya kazi zako, ili utoe chakula katika nchi, na divai imfurahishe mtu moyo wake.

Au:
Yn.6:54

Bwana asema: Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.

SALA BAADA YA KOMUNYO:
Ee Bwana, tunakuomba utuponye kabisa kwa dawa ya huruma yako. Utukamilishe kwa wema wako na kutuhifadhi hivi, hata tuweze kukupendeza katika mambo yote. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu.