DOMINIKA YA 20 YA MWAKA C
MASOMO

ANTIFONA YA KUINGIA: Zab.84:9-10
Ee Mungu, ngao yetu, uangalie, umtazame uso Masiya wako. Hakika siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu.

UTUKUFU husemwa.

KOLEKTA:
Ee Mungu, umewaandalia wakupendao mema yasiyoonekana. Uwashe mioyoni mwetu moto wa upendo wako, ili, kwa kukupenda wewe katika yote na kuliko yote, tuzifikie ahadi zako zinazopita hamu zote. Kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, milele na milele.

SOMO 1: Yer.38:4-6,8-10
Ndipo wakuu wakamwambia mfalme, Twakuomba, mtu huyu auawe, kwa kuwa aidhoofisha mikono ya watu wa vita, waliobaki katika mji huu, na mikono ya watu wote, kwa kuwaambia maneno kama hayo; maana mtu huyu hawatafutii watu hawa heri, bali shari. Naye mfalme Sedekia akasema, tazama, yu mikononi mwenu; maana mfalme siye awezaye kufanya neno lolote kinyume chenu. Basi wakamtwaa Yeremia, wakamtupa katika shimo la Malkiya, mwana wa mfalme, lililo katika uwanda wa walinzi; wakamshusha kwa kamba. Na mle shimoni hamkuwa na maji, ila matope tu; naye Yeremia akazama katika matope hayo. Ebedmeleki akatoka nyumbani mwa mfalme, akamwambia mfalme, akisema, Ee Bwana wangu, mfalme, watu hawa wametenda mabaya katika mambo yote waliyomtenda Yeremia, nabii, ambaye wamemtupa shimoni; naye hakosi atakufa pale alipo, kwa sababu ya njaa; kwa kuwa hapana mkate kabisa katika mji. Ndipo mfalme akamwamuru Ebedmeleki, mkushi, akisema, chukua pamoja nawe watu thelathini; toka hapa, ukamtoe Yeremia shimoni, kabla hajafa.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.40:1-3,17,(K)13
1. Nalimngoja Bwana kwa saburi,
Akaniinamia akakisikia kilio changu.

(K) Ee Bwana, unisaidie hima.

2. Akanipandisha toka shimo la uharibifu,
Toka udongo wa utelezi;
Akaisimamisha miguu yangu mwambani,
Akaziimarisha hatua zangu. (K)

3. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu,
Ndio sifa zake Mungu wetu.
Wengi wataona na kuogopa,
Nao watamtumaini Bwana. (K)

4. Nami ni maskini namhitaji,
Bwana atanitunza.
Ndiwe msaada wangu na wokovu wangu,
Ee Mungu wangu, usikawie. (K)

SOMO 2: Ebr.12:1-4
Wapenzi, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu. Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi.

SHANGILIO: Lk.19:38
Aleluya, aleluya!
Ndiye Mbarikiwa Mfalme ajaye kwa jina la Bwana;
Amani mbinguni, na utukufu huko juu.
Aleluya!

INJILI: Lk.12:49-53
Siku ile Yesu aliwaambia makutano: Nimekuja kutupa moto duniani; na ukiwa umekwisha washwa, ni nini nitakalo zaidi? Lakini nina ubatizo unipasao kubatizwa, nami nina dhiki kama nini hata utimizwe? Je, Mwadhani ya kwamba nimekuja kuleta amani duniani? Nawaambia, La, sivyo, bali mafarakano. Kwa kuwa tokea sasa katika nyumba moja watakuwamo watu watano wamefarakana, watatu kwa wawili, wawili kwa watatu. Watafarakana, baba na mwanawe, na mwana na babaye; mama na binti yake, na binti na mamaye; mkwe mtu na mkwewe; mkwe na mkwe mtu.

Nasadiki husemwa.

MAOMBI
Japo Yesu ameleta amani duniani kwa wanaomuamini, kumfuata Yesu kunaleta utengano na mafarakano kwa baadhi ya watu wasiomuamini.

Ee Bwana Mungu tunaomba,
1. Uwajalie wakubwa na wenye mamlaka serikalini kulinda uhuru wa kubudu kwa wananchi wao.

2. Utuwezeshe kutambua hatari zinazopinga imani yetu na hivyo kuzipinga.

3. Utupe nguvu ya kushinda vishawishi vyote vinavyotuzuia kufuata njia yako.

4. Utupe neema ya kupokea mwito wako wa kukufuata na kukupenda zaidi ya yote.

5. Uwakirimie marehemu wote raha ya milele.

Ee Mungu Mwenyezi, ulitupa amani yako tupate kutofautisha amani yako na kila aina ya amani ya uwongo. Usikilize maombi yetu kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo aliyetupatia amani yako. Amina.

SALA YA KUOMBEA DHABIHU:
Ee Bwana, uvipokee vipaji vyetu vinavyotufanya tushirikiane nawe katika muungano huu mtukufu, ili tunapokutolea vile ulivyotupatia, tustahili kukupokea wewe mwenyewe. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu.

ANTIFONA YA KOMUNYO: Zab.130:7
Kwa Bwana kuna fadhili, na kwake kuna ukombozi mwingi.

Au:
Yn.6:51-52

Bwana asema: Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele.

SALA BAADA YA KOMUNYO:
Ee Bwana, kwa njia ya sakramenti hii tumefanywa washiriki wa Kristo. Tunakuomba kwa unyenyekevu huruma yako, ili, kwa kufanana naye hapa duniani, tustahili kuwa washiriki pamoja naye pia kule mbinguni. Anayeishi na kutawala milele na milele.