JUMANNE JUMA 31 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Rum.12:5-16
Sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya Imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia, kwa bidi; mwenye kurehemu, kwa furaha.Pendo na lisiwe na unafiki; lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana; kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu; kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni, mkijitahidi. Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani. Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao. Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.131
1. Bwana, moyo wangu hauna kiburi, Wala macho yangu hayainuki. Wala sijishughulishi na mambo makuu, Wala na mambo yashindayo nguvu zangu.

(K) Moyo wangu uwe na Amani kwako, Ee Bwana.

2. Hakika nimeituliza nafsi yangu, Na kuinyamazisha. Kama mtoto aliyeachishwa Kifuani mwa mama yake; Ndivyo roho yangu ilivyo kwangu. (K)

3. Ee Israeli, umtarajie Bwana, Tangu leo n ahata milele. (K)

SHANGILIO: Zab.147:12,15
Aleluya, aleluya!
Msifu Bwana, Ee Yerusalemu,
huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya!

INJILI: Lk.14:15-24
Mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja na Yesu alimwambia, Heri yule atakayekula mkate katika ufalme wa Mungu. Akamwambia, Mtu mmoja alifanya karamu kubwa, akaalika watu wengi, akamtuma mtumwa wake saa ya chakula awaambie wale walioalikwa, Njoni, kwa kuwa vitu vyote vimekwisha kuwekwa tayari. Wakaanza wote kutoa udhuru kwa nia moja. Wa kwanza alimwambia, Nimenunua shamba, sharti niende nikalitazame; tafadhali unisamehe. Mwingine akasema, Nimenunua ng’ombe jozi tano, ninakwenda kuwajaribu; tafadhali unisamehe. Mwingine akasema, Nimeoa mke, na kwa sababu hiyo siwezi kuja. Yule mtumwa akaenda, akampa bwana wake habari ya mambo hayo. Basi, yule mwenye nyumba akakasirika, akamwambia mtumwa wake, Toka upesi, uende katika njia kuu na vichochoro vya miji, ukawalete hapa maskini, na vilema, na vipofu, na viwete. Mtumwa akasema, Bwana, hayo uliyoagiza yamekwisha tendeka, na hata sasa ingaliko nafasi. Bwana akamwambia mtumwa, Toka nje uende barabarani na mipakani, ukawashurutishe kuingia ndani, nyumba yangu ipate kujaa. Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu.

--------------

--------------
MAOMBI
Wapendwa, Mungu ndiye mpaji wa neema na karama mbalimbali. Tumwombe katika shida zetu:-

Kiitikio: Pokea ombi letu.
1. Ili wote wanaoitwa kuihubiri Injili na kulihudumia Kanisa lako wasitoe udhuru, bali waupokee wajibu huo kwa moyo mkunjufu. Ee Bwana.

2. Ili wote wenye mamlaka serikalini wasione madaraka kama ni kitu cha kushikamana nacho; bali wawe watumishi wenye utayari hata wa kutoa uhai wao kwa ajili ya wengine. Ee Bwana.

3. Ili ndugu, mali au kitu chochote tulichopewa hapa duniani kitufae kwa wokovu; utuondolee vikwazo kwa miito yetu. Ee Bwana.

4. Ili kila mmoja wetu atumie kipaji alichonacho kwa manufaa ya wengine na kwa sifa na utukufu wako. Ee Bwana.

5. Ili marehemu wetu wakaribishwe kwenye karamu ya uzima wa milele huko mbinguni. Ee Bwana.

Ee Mungu unayetupatia mahitaji yetu na kutuongoza katika kweli yako, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.