JUMANNE JUMA 18 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Hes.12:1-13
Miriamu na Haruni walimnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. Wakasema, Je! ni kweli Bwana amenena na Musa tu? hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao. Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. Bwana akashuka katika nguzo ya wingu, akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. Kisha akawaambia, Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, Bwana, nitajifunua kwake katika maono, nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; kwake nitanena mdomo kwa mdomo, maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake. Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya Hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma. Kisha Haruni akamwambia Musa, Ee bwana wangu. nakusihi sana usituwekee dhambi juu yetu, kwa kuwa tumefanya ya upumbavu, na kufanya dhambi. Nakusihi, asiwe kama mmoja aliyekufa, ambaye nyama ya mwili wake nusu imelika hapo atokapo tumbo la mama yake. Musa akamlilia Bwana, akasema, Mpoze, Ee Mungu, nakusihi sana.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.51:1-5,10-11 (K)1
1. Ee Mungu unirehemu, sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
uyafute makosa yangu.

(K) Ee Mungu uturehemu, kwa kuwa tumefanya dhambi.

2. Unioshe kabisa na uovu wangu,
unitakase dhambi zangu.
Maana nimejua mimi makosa yangu,
na dhambi yangu i mbele yangu daima. (K)

3. Wewe ujulikane kuwa una haki unenapo,
Na kuwa safi utoapo hukumu.
Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu;
Mama yangu alinichukua mimba hatiani. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Shangilio: Zab.19:8
Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi,
huyatia macho nuru.
Aleluya.

INJILI: Mt.15:1-2,10-14
Ndipo Mafarisayo na waandishi toka Yerusalemu walipomwendea Yesu wakisema, Mbona wanafunzi wako huyahalifu mapokeo ya wazee, kwa maana hawanawi mikono walapo chakula. Akawaita makutano akawaambia Sikilizeni, mfahamu; Sicho kiingiacho kinywani kimtiacho mtu unajisi; bali kitokacho kinywani ndicho kimtiacho mtu unajisi. Ndipo wanafunzi wake walipomwendea, wakamwambia, Wajua ya kuwa Mafarisayo walipolisikia neno lile walichukizwa? Akajibu, akasema, Kila pando asilolipanda Baba yangu wa mbinguni litang'olewa. Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.

AU
INJILI: Mt.14:22-36

Yesu aliwalazimisha wanafunzi wake wapande chomboni na kutangulia mbele yake kwenda ng’ambo, wakati yeye alipokuwa akiwaaga makutano. Naye alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake. Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho. Hata wakati wa zamu ya nne ya usiku Yesu akawaendea, akienda kwa miguu juu ya bahari. Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli; wakapiga yowe kwa hofu. Mara Yesu akanena, akawaambia, Jipeni moyo; ni mimi; msiogope. Petro akamjibu, akasema, Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. Akasema, Njoo. Petro akashuka chomboni, akaenda kwa miguu juu ya maji, ili kumwendea Yesu. Lakini alipouona upepo. akaogopa; akaanza kuzama, akapiga yowe, akisema, Bwana, niokoe. Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka? Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia, wakisema, Hakika wewe u Mwana wa Mungu. Na walipokwisha kuvuka, walifika nchi ya Genesareti. Na watu wa mahali pale walipomtambua, walituma watu kwenda nchi zile zilizo kandokando, wakamletea wote waliokuwa hawawezi; nao wakamsihi waguse hata pindo la vazi lake tu; na wote waliogusa wakaponywa kabisa.

--------------

--------------
MAOMBI
Wapendwa, kwa imani na matumaini tumwombe Mungu anayewapa watu utakatifu kama ule wa malaika.

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Viongozi wetu wa Kanisa wazidi kukutambulisha Wewe kwa watu na kuwatangazia neno lako wokovu. Ee Bwana.

2. Uwajalie wote wenye madaraka roho ya kuyapambanua mambo vizuri, wapate kuwatendea haki watu wanaowategemea. Ee Bwana.

3. Utuepushe sisi sote na ukorofi au ubishi wa bure, na kutuamshia imani ya kweli na moyo wa toba. Ee Bwana.

4. Utujalie marafiki wa kweli, wenye kutufaa wakati wa raha na taabu, tupate kuwa watu wako; nawe upate kuwa Mungu wetu pekee. Ee Bwana.

5. Uwaponye wagonjwa; na marehemu wetu wajaliwe uzima wa milele huko mbinguni. Ee Bwana.

Ee Mungu, malaika wanaotuongoza kwenye utakatifu wayapeleke maombi yetu mbele zako. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.