JUMAMOSI JUMA 32 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Hek.18:14-16,19:6-9
Mambo yote yalipokuwa kimya, na usiku ulikuwa katikati ya mwendo wake mwepesi, Neno lako Mwenyezi alishuka mbinguni kutoka kiti chako cha kifalme, shujaa aliye hodari, katika nchi iliyoposishwa hukumu, mwenye upanga mkali, ndio amri yako isiyopindika, akasimama na kujaza mambo yote mauti, na pindi alipogusa mbingu akaikanyaga nchi. Kwa maana ulimwengu mzima, kwa kadiri ya asili yake, ulifanyika tena mpya, kwa kuzitii amri zako hizi na hizi, ili watoto wako walindwe wasipate dhara. Uwingu ulionekana uliokitia uvuli kituo chao, nan chi kavu ikapanda kutoka pale palipokuwapo maji kwanza, katika Bahari ya Shamu kukawa barabara isiyo na zuio, na uwanda wenye majani katika mawimbi yaumkayo. Hapo watu wako wakapita pamoja na majeshi yao yote, ambao kwa mkono wako walifunikwa, wakiisha kuona maajabu makuu. Wakazunguka-zunguka huru kama farasi, wakaruka-ruka kama wana-kondoo, wakikuhimidi Wewe, Bwana, uliyekuwa mkombozi wao.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.105:2-3,36-37,42,43 (K)5
1. Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi, Zitafakarini ajabu zake zote. Jisifuni kwa jina lake takatifu, Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.

(K) Zikumbukeni ajabu Bwana alizozifanya.

2. Akawapiga wazaliwa wa kwanza katika nchi. Malimbuko ya nguvu zao. Akawatoa hali wana fedha na dhahabu, Katika kabila zao asiwepo mwenye kukwaa. (K)

3. Maana alilikumbuka neno lake takatifu, Na Ibrahimu, mtumishi wake. Akawatoa watu wake kwa shangwe, Na wateule wake kwa nyimbo za furaha. (K)

SHANGILIO: Zab.119:105
Aleluya, aleluya!
Neno lako ni taa ya miguu yangu,
na mwanga wa njia yangu.
Aleluya!

INJILI: Lk.18:1-8
Yesu aliwaambia wanafunzi wake mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu siku zote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji Fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima. Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona Imani duniani?

--------------

--------------
MAOMBI
Ndugu, Mungu aliyewakomboa Waisraeli utumwani Misri kwa mkono wa Musa, ndiye aliyetukomboa sisi toka utumwa wa dhambi kwa njia ya Mwanae Yesu Kristo. Kwa maombezi ya Bikira Maria, tumwombe.

Kiitikio: Pokea ombi letu.
1. Ubariki juhudi za Maaskofu na Wakleri wote katika kuhubiri toba iletayo msamaha wa dhambi kwa watu wako. Ee Bwana.

2. Uwe pamoja na viongozi wetu wa serikali ili, hata wafanyapo mikataba na watu wa mataifa mengine, wazilinde mila na desturi zetu njema; tupate kuwa watenda kazi pamoja na kweli. Ee Bwana.

3. Matukio ya kihistoria yanayoonesha nguvu yako kuu dhidi ya yule mwovu na upendo wako mkuu kwa watu wako, yawe kichocheo cha wongofu wa watu wengi. Ee Bwana.

4. Utuongezee ari ya kusali bila kuchoka na udumifu katika kutenda mema tukisukumwa na upendo kwako na kwa wenzetu. Ee Bwana.

5. Ndugu zetu marehemu wasamehewe dhambi zao na kufikishwa huko uliko Wewe. Ee Bwana.

Ee Mungu unayewapatia haki wanaokulilia, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.