JUMAMOSI JUMA 15 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Kut.12:37-42
Wana wa Israeli walisafiri kutoka Ramesesi mpaka Sukothi, walipata hesabu yao kama watu sita mia elfu watu waume waliokwenda kwa miguu, bila kuhesabu watoto. Na kundi kubwa la watu waliochangamana mno wakakwea pamoja nao; na kondoo na ng'ombe, wanyama wengi sana. Nao wakaoka mikate isiyochachwa ya ule unga waliouchukua walipotoka Misri, maana, haukutiwa chachu, kwa sababu walitolewa watoke Misri, wasiweze kukawia, nao walikuwa hawajajifanyia tayari chakula. Basi wana wa Israeli kukaa kwao, maana, muda waliokaa ndani ya Misri, ulikuwa ni miaka mia nne na thelathini. Ilikuwa mwisho wa miaka hiyo mia nne na thelathini, ilikuwa siku ile ile, ya kwamba majeshi yote ya Bwana yalitoka nchi ya Misri. Ni usiku wa kuangaliwa sana mbele za Bwana kwa sababu ya kuwatoa katika nchi ya Misri; huu ndio usiku wa Bwana, ambao wapasa kuangaliwa sana na wana wa Israeli wote katika vizazi vyao.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.136:1,10-15,23-24 (K)1
1. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Yeye aliyewapiga Wamisri kwa kuwaua wazaliwa wa kwanza wao; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Akawatoa Waisraeli katikati yao; Kwa maana fadhili zake ni za milele.

(K) Fadhili zake ni za milele.

2. Kwa mkono hodari na mkono ulionyoshwa; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Yeye aliyeigawa Bahari ya Shamu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Akawavusha Israeli katikati yake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. (K)

3. Aliyetukumbuka katika unyonge wetu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Akatuokoa na watesi wetu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. (K)

SHANGILIO: Yn.14:5
Aleluya, aleluya!
Thoma akamwuliza, “Bwana, hatujui unakokwenda,
tutawezaje basi, kuijua hiyo njia?”
Aleluya!

INJILI: Mt.12:14-21
Mafarisayo walitoka wakafanya shauri juu ya Yesu jinsi ya kumwangamiza. Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; nitatia roho yangu juu yake, naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima, hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.

--------------

--------------
MAOMBI
Ndugu, Yesu Kristo ndiye “Mtumishi wa Bwana" ambaye, kadiri ya nabii Isaya, moyo wa Mungu umependezwa naye. Kwa maombezi ya Bikira Maria mamae, tumwombe tukisema:

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Maaskofu na Mapadre uliowateua kuwa watumishi na watangazaji wa Injili, waimarishwe katika kuutekeleza wajibu huo mkubwa duniani kote. Ee Bwana.

2. Uwaponye wagonjwa na kuwasaidia wote wanaokufuata kwa moyo mnyofu, wakiwa na matatizo mbalimbali ya kimwili na kiroho. Ee Bwana.

3. Utusaidie sisi sote kushika kiaminifu amri zako, kwani ni dira inayotuongoza uliko Wewe. Ee Bwana.

4. Uwaonye wote wanaotumia vibaya mamlaka yao dhidi ya wanyonge; na uwanyenyekeshe wote wenye kukukana na kukudharau Wewe. Ee Bwana.

5. Marehemu wetu wapokelewe kwenye kundi la watakatifu wako huko mbinguni. Ee Bwana.

Ee Kristo Yesu uliyesema mataifa watalitumainia jina lako, uyapokee maombi yetu. Unayeishi na kutawala daima na milele. Amina.