IJUMAA JUMA LA 6 PASAKA
MASIFU YA ASUBUHI
K. Ee Bwana, uifungue midomo yetu.
W. Nasi tutalisifu jina lako.
ANTIFONA YA MWALIKO:
Bwana amefufuka kweli, aleluya.
(K. Ant. ya Mwaliko - W. warudie Ant.)
Zab.95: Utenzi wa kumsifu Mungu
Njoni tumwimbie Mungu;
tumshangilie mwamba wa wokovu wetu!
Tuingie kwake na nyimbo za shukrani;
tumshangilie kwa nyimbo za sifa. (W.Ant.)
Maana Mungu, ni Mungu Mkuu.
Mfalme mkuu juu ya miungu yote.
Dunia yote imo mikononi mwake,
mabonde, na vilele vya milima.
Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya;
nchi kavu kadhalika, yeye aliiumba. (W.Ant.)
Njoni tusujudu na kumwabudu;
tumpigie magoti Mungu, Mwumba wetu!
Maana yeye ni Mungu wetu!
Nasi ni watu anaowalinda,
ni kondoo wake anaowachunga. (W.Ant.)
Laiti leo mngelisikiliza anachosema:
"Msiwe na mioyo migumu kama wazee wenu kule Meriba,
kama walivyokuwa siku ile, kule Masa jangwani!
Huko wazee wenu walinijaribu na kunipima,
ingawa waliyaona mambo niliyowatendea. (W.Ant.)
Kwa miaka arobaini nilichukizwa nao,
nikasema: 'Kweli hawa ni watu waliopotoka!
Hawajali kabisa mwongozo wangu!'
Basi, nilikasirika, nikaapa:
'Hawataingia kwangu wapumzike!' (W.Ant.)
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
kama mwanzo, na sasa, na siku zote na milele.
Amina. (W.Ant.)
UTENZI chagua 1-7
1 (25)
Kristo Bwana amefufuka!
Kila mnyororo Bwana kakata,
Sikilizeni, hao malaika
Makelele kwa shangwe wanapiga,
Milele mbinguni juu waimba,
Aleluya!
Aliyekufa kwa ajili yetu,
Na mateso mengi kuvumilia -
Kuvumilia kwa ajili yetu,
Ni Kondoo wetu wa Paska leo!
Nasi pia kwa shangwe tunaimba.
Aleluya!
Yeye aliyepata maumivu
Na hasara yote msalabani,
Sasa yupo katika utukufu,
Akitwombea, huko mbinguni,
Na anasikia kilio chetu.
Aleluya!
Sasa atuagiza tutangaze
Pote pote ulimwenguni jinsi
Ya kuokoka waliopotea,
Na ya kusamehewa wenye toba,
Na tuwezavyo ingia mbinguni.
Aleluya!
Mikaeli Weisse yapata 1480-1534
2 (26)
Aleluya! Aleluya!
Angani inatanda Pasaka!
Yesu ni mzima, hafi tena!
Giza limetokomezwa lote,
Na Bwana wa nuru Mfufuka!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Mama Maria mwone Mwanao,
Anavyofurahi kwa ushindi!
Mateso mlishiriki nyote,
Milele mtatawala nyote!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Watafuta waliopotea!
Naye Petro anakulilia!
Mwimarishe awe mwamba,
Kundi lako alichunge!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Mzima haishi kaburini,
Kristo yupo ghorofani!
Utukufu wake kauficha,
Mwili wake hai aonesha!
Aleluya! Aleluya!
Aleluya! Aleluya!
Japo uso wake hatuoni,
Yupo na sisi kama mwanzoni!
Ni padre wetu mtukufu,
Twashangilia mtu mzima!
Aleluya! Aleluya!
Yakobo Quinn SJ
3 (27)
Aleluya, mwimbieni Yesu,
Enzi na ufalme ni vyake.
Aleluya, fanaka ni yake,
Ushindi ni wake peke yake.
Sikizeni, nyimbo za Sion
Zinanguruma kama tufani,
Zinasikika kama gharika:
Kwa damu yake ilo azizi,
Yesu ametukomboa sisi,
Watu kutoka kila taifa.
Aleluya, katika huzuni
Kama yatima hatujaachwa;
Aleluya, yu karibu nasi,
Imani yasadiki kabisa,
Haiulizi kwa jinsi gani
Ingawa Bwana alitoweka,
Akafunikwa nayo mawingu
Siku ile ya arobaini,
Tutasahau ahadi yake:
'Nipo nanyi daima milele'?
S. S. Wesley 1810-1876
4 (28)
Kwenye Karamu ya Mwana-Kondoo
Mfalme mshindi twamwimbia,
Alotuosha kwa wingi wa maji
Kutoka penye tobo ubavuni.
Yeye analo pendo la kimungu
Waalikwa wanyweshwa damu yake,
Na awapa waule mwili wake
Pendo ndilo kafara na kuhani.
Panapomwagwa damu ya Pasaka
Mwuaji upanga aufutika;
Jeshi la Israeli lapita
Askari adui wafa maji.
Kristo kondoo aliyechinjwa,
Kafara na mkate wa Pasaka;
Tuile manna itokayo juu
Kwa unyofu na upendo halisi.
Kafara shujaa kutoka juu,
Nguvu za kuzimu ni chini yako;
Vitani mauti umeyashinda,
Uzima na mwanga kutuletea.
Bendera sasa waipeperusha,
Shetani na kaburi watiisha;
Malaika waungana kusifu
Kupinduliwa kwa bwana shetani.
Ushindi na furaha ya Pasaka
Dhambi tu ndo yaweza viharibu;
Tukinge na kifo cha dhambi Bwana,
Tulozaliwa upya ndani yako.
Tenzi za fahari, nyimbo za sifa
Tunakuimbia mpenzi Baba;
Na sifa zote milele mpate,
Bwana Mfufuka na wewe Roho.
Karne ya 7
5 (29)
Utangazeni ushindi wake,
Ewe mbingu na wewe dunia,
Maana Kristo amefufuka
Kama mwenyewe alivyosema:
Ndie yule alosulibiwa,
Ni Mungu kweli aliye hai,
Aliyekaa kwa siku tatu
Kati ya wafu huko kuzimu.
Kristo alikufa kwa aibu
Kwa ajili yetu sisi watu,
Lakini sasa aishi tena
Akiwa na nguvu na uweza;
Moto wake na haujazimwa,
Mwali wake unaoangaza
Ulimwengu wote waujaza
Kwa furaha tele na mwangaza.
Sifa na heshima kwake Baba
Ambaye hakika Hakuumbwa,
Na kwa Mwanae aliye hai
Ambaye hakika hakushindwa,
Bali anatawala kwa enzi
Pamoja na Roho wake Mungu,
Utatu ulio Mtukufu,
Katika yeye Mungu Mmoja.
Stanbrook Abbey Hymnal
6 (30)
Njoni, enyi waamini, njoni,
Mkashangilie kwa furaha;
Mungu kawapa Israeli
Furaha baada ya huzuni;
Wana na binti zake Yakobo
Si watumwa tena wa Farao;
Kawavusha miguu mikavu
Katikati ya Bahari ya Shamu.
Leo ndio roho zachipua;
Kristo jela kabomoa,
Japo siku tatu kawa mfu
Leo kachomoza kama jua;
Kipupwe chote cha dhambi zetu,
Cha muda mrefu na cha kiza,
Metokomezwa kwa yako nuru
Wewe tukusifuye daima.
Milango imara ya mauti,
Wala kaburi pana la giza,
Wala walinzi, wala muhuri,
Havikushiki uwe maiti
Maana leo ulisimama.
Kati yao Kumi na Wawili,
Amani yako ukawapatia
Ipitayo ufahamu wetu.
Mt. Yohane wa Damasko yapata 750
7 (31)
Hakika vita sasa vimekwisha,
Majeshi ya motoni yakimbia;
Tupige ukelele wa ushindi
Kwa furaha na shangwe, aleluya.
Kristo aliyeuvumilia
Ule mti utiao aibu,
Twamkaribisha tukimsifu
Aloshinda mauti, aleluya.
Asubuhi ya tatu kafufuka,
Amevishwa nuru ya utukufu.
Ambayo wenye imani thabiti
Mbinguni watavishwa, aleluya.
Ile milango duni ya kuzimu
Ufunguo wao yaachilia,
Mlango wa Paradisi u wazi;
Tusichoke kuimba, aleluya.
Bwana, kwa mapigo tulokupiga,
Tujalie tuwe mbali na kifo,
Ili tuendelee kukariri
Salamu yetu hii, aleluya.
Simphonia Sirenum 1695
ANT. I: Jipe moyo, mwanangu, umesamehewa dhambi zako, aleluya.
Zab.51 Kuomba msamaha
Jirekebisheni upya rohoni na katika fikra zenu. Vaeni hali mpya ya utu (Ef.4:23-24)
Unihurumie, Ee Mungu,*
kwa sababu ya upendo wako mkuu;
ufutilie mbali uovu wangu,*
kwa sababu ya huruma yako kuu.
Unioshe kabisa kosa langu;*
unisafishe dhambi yangu.
Nakiri kabisa makosa yangu,*
daima naiona waziwazi dhambi yangu.
Nimekukosea wewe peke yako,*
nimetenda yaliyo mabaya mbele yako.
Hivyo wafanya sawa unaponihukumu,*
una haki kabisa unaponiadhibu.
Mimi ni mkosefu tangu kuzaliwa kwangu,*
mwenye dhambi tangu tumboni mwa mama yangu.
Wewe wataka unyofu wa ndani;*
hivyo nifundishe hekima moyoni.
Uniondolee dhambi, nitakate;*
unioshe, niwe mweupe pе.
Hapo nitaweza kufurahi tena;*
nitashangilia tena ingawa uliniponda.
Ugeuze uso wako, usiziangalie dhambi zangu;*
ukayafute makosa yangu yote.
Ee Mungu, uniumbie moyo safi,*
uweke ndani yangu roho mpya na thabiti.
Usinitupe mbali nawe;*
usiniondolee Roho wako mtakatifu.
Unifanye nifurahi tena kwa kuniokoa,*
unijalie moyo radhi wa utii.
Hapo nitawafundisha wakosefu mwongozo wako,*
nao wenye dhambi watarudi kwako.
Ee Mungu, Mungu mwokozi wangu, uniokoe na kifo,*
nami nitatangaza kwa furaha uadilifu wako.
Ifumbue midomo yangu, Ee Bwana,*
nipate kutangaza sifa zako.
Kwa kweli wewe hupendezwi na sadaka,/
ama sivyo mimi ningalikutolea.*
Wewe huna haja na sadaka za kuteketezwa.
Sadaka yangu kwako, Ee Mungu, ni moyo mnyofu;*
wewe, Ee Mungu, hukatai moyo mnyofu na mtiifu.
Ee Mungu, uutendee mji Sion mema:*
jenga tena upya kuta za Yerusalemu.
Hapo utapendezwa na sadaka za kweli;/
dhabihu na sadaka za kuteketezwa*
na fahali watatolewa sadaka madhabahuni pako.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Ant. I: Jipe moyo, mwanangu, umesamehewa dhambi zako, aleluya.
ANT. II: Bwana, ulikuja na nguvu kuwaokoa watu wako; ulikuja na
Kristo wako, aleluya.
WIMBO: Hab.3:2-4,13a,15-19
Simameni na kuinua vichwa vyenu juu, kwa maana ukombozi wenu umekaribia (Lk.21:28)
Ee BWANA, nimesikia habari zako,*
Nami naogopa;
Ee BWANA, fufua kazi yako katikati ya miaka;/
Katikati ya miaka tangaza habari yake; *
Katika ghadhabu kumbuka rehema.
Mungu alikuja kutoka Temani,*
Yeye aliye mtakatifu kutoka mlima Parani.
Utukufu wake ukazifunika mbingu,*
Nayo dunia ikajaa sifa yake.
Mwangaza wake ulikuwa kama nuru;/
Alikuwa na mishale ya nuru ubavuni pake;*
Ndipo ulipofichwa uweza wake.
Ukatokea kwa ajili ya wokovu wa watu wako,*
Kwa ajili ya wokovu wa masihi wako;.
Ukaikanyaga bahari kwa farasi zako,*
Chungu ya maji yenye nguvu.
Nikasikia, na tumbo langu likatetemeka,*
Midomo yangu ikatikisika kwa sauti ile;
Ubovu ukaingia mifupani mwangu,*
Nikatetemeka katika mahali pangu;
Ili nipate kuingoja ile siku ya dhiki,*
Kundi lao washambuliao wakweapo juu ya watu.
Maana mtini hautachanua maua,*
Wala mizabibuni hamtakuwa na matunda;
Taabu ya mzeituni itakuwa bure,*
Na mashamba hayatatoa chakula;
Zizini hamtakuwa na kundi,*
Wala vibandani hamtakuwa na kundi la ng'ombe.
Walakini nitamfurahia BWANA,*
Nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.
BWANA ni nguvu zangu,/
Yeye huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu,*
Naye ataniendesha katika mahali pangu palipoinuka.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
ANT. II: Bwana, ulikuja na nguvu kuwaokoa watu wako; ulikuja na
Kristo wako, aleluya.
ANT. III: Sion, msifu Mungu wako, kwani ameleta amani katika nchi
yako, aleluya.
Zab.147:12-20 Ni vizuri kumsifu Mungu
Njoo! Mimi nitakuonesha bibi arusi, mkewe Mwana-kondoo! (Ufu.21:9)
Ee Yerusalemu, umsifu Mungu!*
Umsifu Mungu wako, ee Sion!
Maana ameiimarisha milango yako,*
amewabariki watu waliomo kwako.
Ameweka amani mipakani mwako;*
anakushibisha kwa ngano safi kabisa.
Yeye hupeleka amri yake duniani,*
na neno lake hutekelezwa upesi.
Hutandaza theluji kama pamba,*
hutawanya umande kama majivu.
Huleta mvua ya mawe/
vipande vikubwa vikubwa kama mkate*
na kwa ubaridi wake maji huganda.
Kisha hutoa amri, na maji hayo huyeyuka;*
huvumisha upepo wake, nayo hutiririka.
Humjulisha Yakobo ujumbe wake,*
na Israeli amri na maagizo yake.
Lakini watu wengine hakuwafanyia hayo;*
watu wengine hawayajui maagizo yake.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
ANT. III: Sion, msifu Mungu wako, kwani ameleta amani katika nchi
yako, aleluya.
SOMO: Mate.5:30-32
Mungu wa babu zetu alimfufua Yesu baada ya ninyi kumwua kwa kumtundika msalabani. Huyu ndiye
yule aliyekwezwa na Mungu mpaka upande wake wa kulia, akawa Kiongozi na Mkombozi, ili awawezeshe
watu wa Israeli kutubu, wapate kusamehewa dhambi zao. Sisi ni mashahidi wa tukio hilo, naye Roho
Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wale wanaomtii, anashuhudia pia tukio hilo.
KIITIKIZANO
K. Bwana amefufuka kutoka wafu, aleluya, aleluya. (W. Warudie)
K. Kwa ajili yetu alikufa msalabani.
W. Aleluya, aleluya.
K. Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu.
W. Bwana...
Ant. Wimbo wa Zakaria
Katika Yesu tunamwona Yeye ambaye amevikwa sasa taji ya utukufu na heshima, kwa sababu
aliuawa, aleluya.
WIMBO WA ZAKARIA
Lk.1:68-79 Masiha na mtangulizi wake
Asifiwe Bwana Mungu wa Israeli,/
kwani amekuja kuwasaidia*
na kuwakomboa watu wake.
Ametupatia Mwokozi shujaa,*
mzao wa Daudi, mtumishi wake.
Aliahidi hapo kale*
kwa njia ya manabii wake watakatifu,
kwamba atatuokoa kutoka maadui wetu*
na kutoka mikono ya wote wanaotuchukia.
Alisema kwamba atawaonea huruma wazee wetu,*
na kukumbuka agano lake takatifu.
Kwa kiapo alichomwapia mzee wetu Abrahamu/
aliahidi kutukomboa kutoka maadui wetu*
na kutujalia tumtumikie bila hofu,
ili tuwe watakatifu na waadilifu mbele yake*
siku zote za maisha yetu.
Nawe, mwanangu, utaitwa:*
nabii wa Mungu Aliye Juu,
utamtangulia Bwana*
kumtayarishia njia yake;
kuwatangazia watu kwamba wataokolewa*
kwa kuondolewa dhambi zao.
Mungu wetu ni mpole na mwenye huruma,/
atasababisha pambazuko angavu la ukombozi*
litujie kutoka juu,
na kuwaangazia wote wanaokaa/
katika giza kuu la kifo,*
aongoze hatua zetu katika njia ya amani.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Ant. Katika Yesu tunamwona Yeye ambaye amevikwa sasa taji ya utukufu
na heshima, kwa sababu aliuawa, aleluya.
MAOMBI
Kwa njia ya Roho wake, Mungu alimfufua Yesu kutoka wafu. Na ataipatia uzima miili yetu ya
kibinadamu. Tumwombe, tukisema:
W. Bwana, utupatie uzima kwa njia ya Roho wako Mtakatifu.
Baba, uliikubali sadaka ya Mwanao, ukamfufua kutoka wafu;
- uyapokee matoleo yetu ya asubuhi, na utuongoze kwenye uzima wa milele. (W.)
Udhihirishe uwepo wako katika kazi zetu za leo;
- na tufanye kila kitu kwa ajili ya utukufu wako, na kwa ajili ya kuutakatifuza ulimwengu
wetu. (W.)
Usiruhusu kazi zetu zipotee bure,
- bali ziwafae wenzetu, na kutufikisha kwenye ufalme wako. (W.)
Yafumbue macho yetu, tuweze kutambua shida za ndugu zetu;
- iamshe mioyo yetu, tuweze kuwapatia upendo wetu. (W.)
Sala ya Baba yetu:
K. Tunapoungojea ujio wa utawala wa Mungu, tusali tukisema:
Baba Yetu...
Baba Yetu, uliye mbinguni,
jina lako litukuzwe.
Ufalme wako ufike.
Utakalo lifanyike, duniani kama mbinguni.
Utupe leo mkate wetu wa kila siku;
utusamehe makosa yetu,
kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea,
usitutie katika kishawishi,
lakini utuopoe maovuni. Amina.
SALA:
Bwana, isikie sala yetu. Umtume kwa watu wote Roho anayetufanya tuwe wana wako, kama alivyobashiri
Kristo, shahidi wa ukweli wako: na hivi uikamilishe, kwa njia ya injili, kazi ya kutakatifuza,
iliyoahidiwa na Neno wako. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, Mwanao, anayeishi na
kutawala nawe na Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele.
W. Amina.
K. Bwana atubariki, atukinge na maovu yote, na atufikishe kwenye uzima wa milele.
(W.) Amina.