IJUMAA JUMA 32 LA MWAKA WA 1
MASOMO
SOMO 1: Hek.13:1-9
Bila shaka wanadamu wote kwa asili ni ubatili, ambao hawana akili za kumtambua Mungu; tena hawakupata
uwezo wa kumjua yeye aliopo kwa kuvitazama viumbe vizuri vinavyoonekana, wala kwa kuyaangalia
yaliyofanywa hawakufahamu yule fundi aliyeyafanya. Walakini moto, ama upepo, ama hewa nyepesi, ama
mzunguko wa nyota, ama mafuriko ya maji, ama mianga ya mbinguni walidhania kuwa ni miungu inayoutawala
ulimwengu! Huenda ilikuwa kwa kupendezwa na uzuri wake walivyodhania viumbe hivyo kuwa ni miungu,
basi na wajue kadiri gani Bwana, Mfalme wao avipitiavyo; kwa maana yeye aliye asili ya uzuri ndiye
aliyeviumba. Lakini kama ilikuwa kwa kuzistaajabia nguvu zake na maongozi yake, na wafahamu kwa
kuviangalia kadiri gani yeye aliyeviumba anayo nguvu zaidi; maana kwa jinsi uzuri hata wa viumbe
vilivyoumbwa ulivyo mkuu, kwa kadiri iyo hiyo mwanadamu huyatunga mawazo yake juu ya Muumba. Walakini
watu hao hawana hatia nyingi. Madhali yawezekana kwamba hao wamekosea tu, pindi wanapomtafuta Mungu,
na kutamani kumwona; kwa sababu huishi katikati ya viumbe vyake, huvichunguza kwa bidii, na mwisho
hujitoa kwa maono yao, mradi vitu vyenyewe wanavyovitazama ni vizuri kweli kweli. Walakini tena watu
hao hawana udhuru. Kwa maana ya viumbe, imekuwaje ya kwamba hawakudiriki upesi kumtambua Mfalme Mkuu
wa viumbe hivyo vyake?
WIMBO WA KATIKATI: Zab.19:1-4 (K)1
1. Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu,
Na anga laitangaza kazi ya mikono yake.
Mchana husemezana na mchana,
Usiku hutolea usiku maarifa.
(K) Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu.
2. Hakuna lugha wala maneno,
Sauti yao haisikilikani.
Sauti yao imeenea duniani mwote,
Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. (K)
SHANGILIO: Zab.111:7,8
Aleluya, aleluya!
Maagizo yako yote, Ee Bwana, ni amini,
yamethibitika milele na milele.
Aleluya!
INJILI: Lk.17:26-37
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika
siku zake Mwana wa Adamu. Walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakioa na kuolewa, hata siku
ile Nuhu aliyoingia katika safina, gharika ikashuka ikawaangamiza wote. Na kadhalika, kama
ilivyokuwa katika siku za Lutu, walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda
na kujenga; lakini siku ile Lutu aliyotoka Sodoma kulikunya moto na kibiriti kutoka mbinguni
vikawaangamiza wote. Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu. Katika
siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na
kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma. Mkumbukeni mkewe Lutu. Mtu yeyote atakaye kuiponya
nafsi yake, ataiangamiza; na yeyote atakayeiangamiza ataiponya. Nawaambia, usiku huo watu wawili
watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. Wanawake wawili watakuwa wakisaga
pamoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. Wakajibu, wakamwuliza, Wapi, Bwana? Akawaambia. Ulipo
mzoga, ndipo watakapokutanika tai.
--------------
--------------
MAOMBI
Ee Mungu, Mwanao amesema ulipo mzoga ndipo
watakapokutanika tai. Sisi tuliokusanyika hapa kwa
jina lake, twakuomba:-
Kiitikio: Upokee ombi letu.
1. Viongozi wetu wa Kanisa wasichoke kuwakumbusha
watu wako juu ya ujio wa Mwanao siku ya mwisho. Ee Bwana.
2. Utawale mioyo ya viongozi wote wa serikali, ili
wasiruhusu nchini dini haramu au vikundi vya matapeli na
wadanganyifu; bali wasimamie utu wema, haki, ukweli na
amani. Ee Bwana.
3. Wote wasiokufahamu wapate kukiri uwepo wako,
walao kwa kuvitazama viumbe vizuri vinavyoonekana,
na kwa kuzichungulia taratibu za viumbe hivyo. Ee Bwana.
4. Sisi tunaomwamini Mwanao Yesu Kristo tujaliwe
kuikiri imani yetu kwa maneno na matendo yetu mema siku
zote. Ee Bwana.
5. Marehemu wetu wasamehewe dhambi zao na
kufikishwa kwako huko mbinguni. Ee Bwana.
Ee Mungu unayetaka tuwe tayari hata kuziangamiza nafsi
zetu kwa ajili yako, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya
Kristo Bwana wetu. Amina.