IJUMAA JUMA 14 LA MWAKA WA 1
MASOMO
SOMO 1: Mwa.46:1-7,28-30
Israeli alisafiri pamoja na yote aliyokuwa nayo, akaja Beer-sheba, akamchinjia sadaka Mungu wa Isaka
babaye. Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa.
Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa
kubwa huko. Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha lena bila shaka; na Yusufu
ataweka mkono wake juu ya macho yako. Yakobo akaondoka kutoka Beer-sheba; wana wa Israeli wakamchukua
baba yao, na watoto wao wadogo, na wake zao katika magari aliyoyapeleka Farao ili kumchukua. Wakatwaa
na wanyama wao, na mali zao walizokuwa wamezipata katika nchi ya Kanaani, wakaja Misri, Yakobo na
uzao wake wote pamoja naye. Wanawe, na wana wa wanawe, pamoja naye, binti zake na binti za wanawe,
na uzao wake wote, aliwaleta pamoja naye mpaka Misri. Yakobo akampeleka Yuda mbele yake kwa Yusufu,
ili amwongoze njia mpaka Gosheni. Wakaja mpaka nchi ya Gosheni. Yusufu akatandika gari lake, akapanda
kwenda kumlaki Israeli, babaye, huko Gosheni; akajionyesha kwake, akamwangukia shingoni, akalia
shingoni mwake, kitambo kizima. Israeli akamwambia Yusufu, Na nife sasa, kwa kuwa nimekuona uso
wako, ya kuwa ungali hai.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.37:3-4,18-19,27-28,39-40 (K)39
1. Umtumaini Bwana ukatende mema,
ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu.
Nawe utajifurahisha kwa Bwana,
naye atakupa haja za moyo wako.
(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.
2. Bwana anazijua siku za wakamilifu,
na urithi wao utakuwa wa milele.
Hawataaibika wakati wa ubaya,
na siku za njaa watashiba. (K)
3. Jiepue na uovu, utende mema,
na kukaa hata milele.
Kwa kuwa Bwana hupenda haki,
wala hawaachi watauwa wake. (K)
4. Na wokovu wenye haki una Bwana,
Yeye ni ngome yao wakati wa taabu.
Naye Bwana huwasaidia na kuwaopoa,
huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa,
kwa kuwa wamemtumaini Yeye. (K)
SHANGILIO: Yak.1:21
Aleluya, aleluya!
Pokeeni kwa upole neno la Mungu
lililopandwa ndani,
liwezalo kuziokoa roho zenu.
Aleluya!
INJILI: Mt.10:16-23
Yesu aliwaambia mitume wake: Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa mwitu; basi
iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua. Jihadharini na wanadamu; kwa maana
watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali
na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka,
msifikirifikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao,
bali ni Roho wa Baba yenu ndani yenu. Na ndugu atamsaliti nduguye ili auawe, na baba atamsaliti
mwana, na wana watawainukia wazazi wao, na kuwafisha. Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa
ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. Lakini watakapowafukuza
katika mji huu, kimbilieni mwingine; kwa maana ni kweli nawaambia, Hamtaimaliza miji ya Israeli,
hata ajapo Mwana wa Adamu.
--------------
--------------
MAOMBI
Ndugu, maisha ni safari yenye hatari nyingi. Kwa vile
sisi ni wasafiri tunaohitaji msaada wa Mungu, tuombe.
Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Viongozi wa Kanisa wajaliwe ujasiri wa kunena na
kutenda matendo yako makuu, kwa nguvu ya
Roho wako Mtakatifu, dhidi ya maadui wa imani
yetu. Ee Bwana.
2. Watawala wa dunia waheshimu uhuru wa dini na
kuwachukulia hatua za kisheria wote wanaovuruga
amani na kukiuka haki za binadamu. Ee Bwana.
3. Utuondolee maovu yote; na daima utukumbushe
kuwa njia zako zimenyooka, nao wenye haki
watakwenda katika njia hizo; bali waasio
wataanguka ndani yake. Ee Bwana.
4. Utuepushe na usaliti; aidha utujalie upendo wa kweli
na ari ya kuwa tayari kuteswa, kwa ajili ya kutangaza
Injili yako popote ulimwenguni. Ee Bwana.
5. Wagonjwa wetu wajaliwe uvumilivu na afya njema;
na marehemu wetu wapokelewe katika makao yako
ya milele huko mbinguni. Ee Bwana.
Ee Mungu uliyezisikiliza sala za Mwanao hata alipokuwa
msalabani, uzipokee sala zetu katika adhimisho hili. Kwa
njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.