IJUMAA JUMA 11 LA MWAKA WA 1
MASOMO
SOMO 1: 2Kor.11:18,21-30
Wengi wanajisifu kwa jinsi ya mwili, mimi nami nitajisifu. Nanena kwa jinsi ya kujidhili kana kwamba
sisi tulikuwa dhaifu. Walakini, akiwa mtu anao ujasiri kwa lo lote, (nanena kipuuzi), mimi nami ninao
ujasiri. Wao ni Waebrania? Na mimi pia. Wao ni Waisraeli? Na mimi pia. Wao ni uzao wa Ibrahimu? Na
mimi pia. Wao ni wahudumu wa Kristo? (Nanena kiwazimu), mimi ni zaidi; katika taabu kuzidi sana;
katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi. Kwa Wayahudi mara
tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa
mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara
nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang'anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine;
hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na
masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi
na kuwa uchi. Baghairi ya mambo ya nje, yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa yote.
Ni nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe? Ikinibidi kujisifu,
nitajisifia mambo ya udhaifu wangu.
WIMBO WA KATIKATI: Zab.34:1-6 (K)17
1. Nitamhimidi Bwana kila wakati,
Sifa zake zi kinywani mwangu daima.
Katika Bwana nafsi yangu itajisifu,
Wanyenyekevu wasikie wakafurahi.
(K) Wenye haki Bwana anawaponya na taabu zao zote.
2. Mtukuzeni Bwana pamoja nami,
Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
Nalimtafuta Bwana akanijibu,
Akaniponya na hofu zangu zote. (K)
3. Wakamwelekea macho wakatiwa nuru,
Wala nyuso zao hazitaona haya.
Maskini huyu aliita, Bwana akasikia,
Akamwokoa na taabu zake zote. (K)
SHANGILIO: Zab.25:4,5
Aleluya, aleluya!
Ee Bwana uniongoze katika ukweli wako
na kunifundisha.
Aleluya!
INJILI: Mt.6:19-23
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi
huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala
wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako. Taa
ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho
lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza;
si giza hilo!
--------------
--------------
MAOMBI
Ndugu, miito yetu inasongwa na hatari nyingi. Hata
Bwana wetu Yesu Kristo alipata mateso mengi mpaka
akafa msalabani. Kwa vile utume wetu unahitaji
msaada wa Mungu, tuombe:-
Kiitikio: Upokee ombi letu.
1. Tunamwombea Askofu wetu F., ili azidi
kuwahamasisha waamini katika kuitunza imani safi
na kuitetea kwa gharama yoyote. Ee Bwana.
2. Uwajalie viongozi wetu kutumia vema elimu na
vipawa vyote walivyojaliwa, ili watu wao waondokane
na giza la ujinga na udanganyifu. Ee Bwana.
3. Walezi wote katika taasisi za malezi wawe mfano
bora kwa walelewa; wakitumia vipaji vyao kwa
ajili ya sifa na utukufu wako. Ee Bwana.
4. Sisi sote tujaliwe kuona fahari juu ya mateso au
magumu tunayoyapata kwa ajili ya imani yetu na
huduma zetu kwa wenye shida. Ee Bwana.
5. Kwa mateso ya Mwanao, wagonjwa wetu wapate
kitulizo na faraja; na kwa ufufuko wake, marehemu
wetu wapate uzima usio na mwisho. Ee Bwana.
Ee Mungu, Wewe unastahili sifa na shukrani zetu. Upokee
sala yetu, kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.