ALHAMISI JUMA 24 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: 1Tim.4:12-16
Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi. Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee. Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote. Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.111:7-10 (K)2
1. Matendo ya mikono yake ni kweli na hukumu, Maagizo yake yote ni amini, Yamethibitika milele na milele, Yamefanywa katika kweli na adili.

(K) Matendo ya Bwana ni makuu.

2. Amewapelekea watu wake ukombozi, Ameamuru agano lake liwe la milele, Jina lake ni takatifu la kuogopwa. (K)

3. Kumcha Bwana ndio mwanzo wa hekima, Wote wafanyao hayo wana akili njema, Sifa zake zakaa milele. (K)

SHANGILIO: Zab.119:11
Aleluya, aleluya!
Nimeshika neno lako moyoni mwangu,
nisije nikakukosea.
Aleluya!

INJILI: Lk.7:36-50
Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika Yesu ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani. Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu. Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu. Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi. Yesu akajibu akamwambia, Simoni, nina neno nitakalo kukuambia. Akasema, Mwalimu, nena. Akasema, Mtu mmoja mkopeshaji alikuwa na wadeni wawili; mmoja amwia dinari mia tano, na wa pili hamsini. Nao walipokuwa hawana cha kumlipa, aliwasamehe wote wawili. Katika hao wawili ni yupi atakayempenda zaidi? Simoni akajibu akasema, Nadhani ni yule ambaye alimsamehe nyingi. Akamwambia, Umeamua haki. Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu; na hakuacha kunibusu sana miguu yangu. Hukunipaka kichwa changu mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu. Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo. Kisha alimwambia mwanamke, Umesamehewa dhambi zako. Ndipo wale walioketi chakulani pamoja naye walianza kusema mioyoni mwao, Ni nani huyu hata asamehe dhambi? Akamwambia yule mwanamke, Imani yako imekuokoa, enenda zako kwa amani.

--------------

--------------
MAOMBI
Wapendwa, kwa vile sisi sote ni watenda kazi katika shamba la Bwana, kwa imani tumpelekee Mungu maombi yetu.

Kiitikio: Pokea ombi letu.
1. Maaskofu na Mapadre wetu wasiache kuitumia karama ya unabii iliyomo ndani yao, ili wawe kielelezo kwa waamini wao katika usemi na mwenendo, katika upendo, na katika imani na usafi. Ee Bwana.

2. Viongozi wa serikali watoe fursa kwa waamini kukuabudu Wewe Mungu, ili neno lako lipate kuenea na kuziokoa nafsi za watu wako. Ee Bwana.

3. Utuongezee sisi sote imani katika ukuu wako na katika uwezo wako wa kuponya roho na mwili. Ee Bwana.

4. Tunawaombea matajiri, ambao kwa neema ya Mungu wamekuwa kama walivyo, ili wazitumie karama walizopewa kwa kulisaidia Kanisa na wote wenye shida. Ee Bwana.

5. Uziokoe roho za ndugu zetu marehemu, wapate kufika huko mbinguni na kukusifu milele. Ee Bwana.

Ee Mungu uliyetupatia imani iletayo wokovu, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.