ALHAMISI JUMA 18 LA MWAKA WA 1
MASOMO

SOMO 1: Hes.20:1-13
Wana wa Israeli, mkutano wote, wakaingia bara ya Sini, katika mwezi wa kwanza, watu wakakaa Kadeshi; Miriamu akafa huko, akazikwa huko. Na hapo hapakuwa na maji kwa ule mkutano; wakajikusanya juu ya Musa na juu ya Haruni. Watu wakashindana na Musa, wakanena, wakisema, Ingalikuwa heri kama tungalikufa wakati ule ndugu zetu walipokufa mbele za Bwana! Mbona mmewaleta kusanyiko la Bwana hata jangwa hili ili tufe huku, sisi na wanyama wetu? Na mbona mmetupandisha kutoka Misri ili kutuleta hata mahali hapa pabaya? Si mahali pa mbegu, wala tini, wala mizabibu, wala makomamanga; wala hapana maji ya kunywa. Musa na Haruni wakatoka pale palipokuwa mkutano, wakaenda hata mlangoni pa hema ya kukutania, wakaanguka kifudifudi; utukufu wa Bwana ukawatokea. Bwana akasema na Musa, akinena, Twaa ile fimbo, ukawakusanye mkutano, wewe na Haruni ndugu yako, ukauambie mwamba mbele ya macho yao utoe maji yake, nawe utawatokezea maji katika mwamba, na hivyo utawanywesha maji mkutano na wanyama wao. Musa akaitwaa hiyo fimbo kutoka mbele za Bwana kama alivyomwamuru. Musa na Haruni wakawakusanya kusanyiko mbele ya mwamba, akawaambia, Sikieni sasa, enyi waasi; je! Tuwatokezee maji katika mwamba huu? Musa akainua mkono wake akaupiga ule mwamba kwa fimbo yake mara mbili; maji yakatoka mengi, mkutano wakanywa na wanyama wao pia. Bwana akamwambia Musa na Haruni, Kwa kuwa hamkuniamini mimi, ili kunistahi mbele ya macho ya wana wa Israeli, basi kwa sababu hiyo, hamtawaingiza kusanyiko hili katika ile nchi niliyowapa. Maji haya ni maji ya Meriba; kwa sababu wana wa Israeli waliteta na Bwana, naye alijionyesha kuwa mtakatifu kati yao.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.95:1-2,6-9 (K)8
1. Njoni, tumwimbie Bwana, Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu. Tuje mbele zake kwa shukrani, Tumfanyie shangwe kwa zaburi.

(K) Ingekuwa heri msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu.

2. Njoni, tuabudu, tusujudu, Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, Na sisi tu watu wa malisho yake, Na kondoo za mkono wake. Ingekuwa heri leo msikie sauti yake! (K)

3. Msifanye migumu mioyo yenu; Kama vile huko Meriba Kama siku ya Masa jangwani. Hapo waliponijaribu baba zenu, Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)

SHANGILIO: zab.130:5
Aleluya, aleluya!
Roho yangu inamngoja Bwana
na Neno lake nimelitumainia
Aleluya!

INJILI: Mt.16:13-23
Yesu alienda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa ni nani? Wakasema, Wengine hunena u Yohane Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii. Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani? Simony Petro akajibu akasema, Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lolote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lolote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni. Ndipo aliwakataza sana wanafunzi wake wasimwambie mtu yeyote ya kwamba yeye ndiye Kristo. Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazia yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.

--------------

--------------
MAOMBI
Ndugu wapendwa, Mungu anajionesha kuwa ni Mtakatifu hata pale mwanadamu anaposhindwa kumjua alivyo, kumtii na kumkiri mbele ya watu. Kwa hiyo, tumwombe.

Kiitikio: Twakuomba utusikie.
1. Umjalie Baba Mtakatifu wetu F. na Maaskofu wote kuyatumia vema na kwa ujasiri mamlaka waliyopewa, ya kuliongoza na kulilinda Kanisa lako. Ee Bwana.

2. Uwajalie watawala wa dunia kuyatatua matatizo ya kijamii kwa njia za haki na amani. Ee Bwana.

3. Utujalie sisi sote kudumu katika uaminifu na imani thabiti kwako, hata tunapopatwa na mateso au majaribu dhidi ya utume wetu. Ee Bwana.

4. Ekaristi Takatifu iwajalie nguvu ya kudumu kiaminifu, wale waliofanya maagano matakatifu mbele yako na mbele ya Kanisa. Ee Bwana.

5. Uwapumzishe ndugu zetu marehemu katika ufalme wako huko mbinguni. Ee Bwana.

Ee Mungu uliyependa kukaa kati yetu katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, uyapokee maombi yetu. Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.