Generic placeholder image
Tarehe 26 Julai

WAT. YOAKIM NA ANNA
MASOMO

SOMO: Ybs.44:1,10-15
Haya na tuwasifu watu wa utauwa, Na baba zetu katika vizazi vyao. Lakini hawa walikuwa watu wa utauwa, wala kazi zao za haki hazisahauliki. Wema wao utawadumia wazao wao, Na urithi wao una wana wa wana; Wazao wao wanashikamana na agano, Na watoto wao kwa ajili yao. Kumbukumbu lao litadumu milele, Wala haki yao haifutiki kamwe; Miili yao imezikwa katika amani, Na jina lao laishi hata vizazi vyote. Mkutano wa watu wataitangaza hekima yao, Na makusanyiko watazihubiri sifa zao.

WIMBO WA KATIKATI: Zab.132:11,13-14,17-18(K)Lk.1:32
1. Bwana amemwapia Daudi neno la kweli,
Hatarudi nyuma akalihalifu,
Baadhi ya wazao wa mwili wako
Nitawaweka katika kiti chako cha enzi.

(K) Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi,
baba yake.

2. Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni,
Ameitamani akae ndani yake.
Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele,
Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani. (K)

3. Hapo nitamchipushia Daudi pembe,
Na taa nimemtengenezea masihi wangu.
Adui zake nitawavika aibu,
Bali juu yake taji yake itasitawi. (K)

SHANGILIO:
Aleluya, aleluya!
Waliitarajia faraja ya Israeli,
na Roho Mtakatifu alikuwa juu yao.
Aleluya!

INJILI: Mt.13:16-17
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia. Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie.

MAOMBI
Ndugu zangu, Mungu ametupenda akamtuma mwanaye Bwana Yesu Kristo ambaye alitupenda mpaka kufa na kutupa amri kuu ya upendano. Tunaomba,

1. Kwa maombezi ya Watakatifu Yoakim na Anna uamshe ndani yetu hamu ya kukupenda wewe na kuwapenda wenzetu kwa matendo.

2. Uwafanye watumishi wote wa Kanisa wawe wachungaji wanaowahurumia watu wanyonge hasa maskini na wanaonewa.

3. Uwajaze waumini wote mioyo ya kuwa wajumbe wa upendo wako.

4. Uamshe ndani yetu moyo wa kuwa karibu na wagonjwa mahututi na wale wote walioachwa na jamaa kuwasaidia.

5. Uwapelekee watoto yatima na wajane wajumbe wa upendo wako.

Ee Bwana Yesu ulisema: Mliyomtendea mmojawapo wa wadogo mmenitendea mimi. Kwa maombezi ya Watakatifu Yoakim na Anna, utufungue macho yetu tuwaone wote wanaohitaji msaada wetu, unayeishi na kutawala pamoja na Mungu Baba katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu daima na milele. Amina.