MT. ANTONI WA PADUA
Padre na mwalimu wa kanisa
SALA ZA MCHANA
chagua SALA KABLA YA ADHUHURI
chagua SALA BAADA YA ADHUHURI
Kwa SALA YA ADHUHURI: endelea hapo chini
ADHUHURI
K. Ee Mungu, uje kutusaidia.
W. Ee Bwana, utusaidie hima.
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo, na sasa, na siku zote, na milele.
Amina.
UTENZI
E Bwana Mbarikiwa
Mungu Muumbaji wetu,
Vitu vyote hutakaswa
Katika Wewe, E Mungu,
Wewe waviimarisha
Hata milele vidumu.
Wenye heri, e mkono
Mtakatifu wa Mungu,
Ndiwe watakatifuza
Vitu vyote, vyote vitu,
Na upya unavitia
Wavipamba vyasitawi.
Ewe fahari tukufu,
Enzi yake Bwana Mungu,
Ndani mwako wachukua
Vyote unavyovijaza;.
Na yote yanafanyika.
Kadiri unavyotaka.
Usifiwe, utukuzwe
Utatu Mtakatifu,
Ujuaye kwa hakika
Na makini zako njia;
Wewe ndiwe nuru kuu.
Milele inayodumu.
ANT: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea
mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).
Zab.123 Kuomba huruma
Wale vipofu wawili walipaaza sauti wakisema, Mheshimiwa, Mwana wa Daudi, utuonee huruma!
(Mt.20:30)
Ninakuinulia macho yangu, Ee Mungu*
unayekaa huko juu mbinguni.
Kama watumishi wamtegemeavyo bwana wao,*
kama mjakazi amtegemeavyo bibi yake,
ndivyo tunavyokutegemea wewe, Ee Mungu, Mungu wetu,*
mpaka hapo utakapotuonea huruma.
Utuhurumie, Ee Mungu, utuhurumie,*
maana tumedharauliwa mno.
Tumedharauliwa na wadhalimu wenye kiburi,*
tumepuuzwa vya kutosha na matajiri.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Zab.124 Mungu kinga yetu
Bwana alimwambia Paulo katika ono: 'Usiogope,...maana mimi nipo pamoja nawe'
(Mate.18:9-10)
Haya Israeli, sasa useme:*
"Kama Mungu asingalikuwa upande wetu;
kweli Mungu asingalikuwa upande wetu,*
wakati ule tuliposhambuliwa na watu,
hakika tungalimezwa wazimawazima,*
wakati hasira zao zilipotuwakia.
Hapo tungalikumbwa na gharika/
tungalifunikwa na mto wa maji,*
mkondo wa maji ungalituchukua!"
Atukuzwe Mungu,*
asiyetuacha makuchani mwao.
Tumeponyoka kama ndege*
katika mtego wa wawindaji!
Mtego umeteguliwa,*
nasi tukaokoka.
Msaada wetu watoka kwa Mungu,*
aliyeumba mbingu na dunia.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
Zab.125 Usalama wa watu wa Mungu
Amani na iwe kwa Israeli - Wateule wa Mungu (Gal.6:16)
Wale wanaomtumainia Mungu,/
ni kama mlima Sion,*
ambao hautikisiki, bali uko imara daima.
Kama Yerusalemu inavyozungukwa na milima,/
ndivyo Mungu awazungukavyo watu wake,*
tangu sasa na hata milele.
Maana hatawaruhusu waovu watawale nchi ya waadilifu;*
Wasije waadilifu nao wakafanya maovu.
Ee Mungu, uwe mwema kwa watu wema,*
kwa wale wanaozitii amri zako.
Adhabu unayowapa watu waovu*
uwape pia wanaokiuka miongozo yako.
Atukuzwe Baba na Mwana*
na Roho Mtakatifu.
Kama mwanzo na sasa na siku zote*
na milele. Amina
ANT: Mtu anayewapokea ninyi, hunipokea mimi: yeyote anayenipokea
mimi, humpokea Yeye aliyenituma (aleluya).
SOMO: 1Tim.1:12
Namshukuru Bwana wetu Yesu Kristo, aliyenipa nguvu kwa ajili ya kazi yangu. Namshukuru kwa
kuniona mimi kuwa ni mwaminifu, akaniteua nimtumikie.
K. Sitaona aibu kutangaza Habari Njema (aleluya).
W. Uwezo wa Mungu ndio unaowaokoa watu (aleluya).
SALA:
Tuombe: Mungu Mwenyezi wa milele, uliwapatia watu wako Mtakatifu Antoni wa Padua awe mhubiri
wako maarufu, na msaidizi katika shida zao. Utujalie, kwa msaada wake, tuweze kuishi vema kikristo,
na kutambua kuwa wewe unatusaidia katika majaribu yetu yote. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristo
Bwana wetu.
W. Amina.
K. Tumtukuze Bwana.
(W.) tumshukuru Mungu.